Friday, July 8, 2011

Mamlaka ya Mikoa kwa mujibu wa sheria

Rais wa Zanzibar ana madaraka chini ya kifungu cha 4 (1) cha sheria ya tawala za Mikoa, kumteua Mkuu wa Mkoa kwa kila Mkoa uliopo ndani ya Zanzibar.
Kazi za Mkuu wa Mkoa zimeelezwa chini ya kifungu cha 5 cha Sheria ya Tawala za Mikoa kuwa ni:-
(i). kuangalia, kusimamia na kusaidia katika utendaji wa shughuli za Serikali ndani ya Mkoa wake;
(ii). kuhakikisha kuwa Sera, mipango na maelekezo ya Serikali yanafuatwa;
(iii). kusimamia amani na utawala wa Sheria katika Mkoa wake kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi; na
(iv). kuhakikisha kuwa nyenzo za Serikali (ambazo ni vifaa au mali na watu) zinatumika ipasavyo kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Aidha katika kuhakikisha hali ya amani na usalama katika Mkoa
wake, Mkuu wa Mkoa ana uwezo wa kumkamata na kumuweka kuzuizuini mtu yeyote au kuamrisha polisi kwa maandishi kumkamata mtu yeyote na kumuweka kizuini, endapo kuna ushahidi kuwa mtu huyo anavunja amani au anaelekea kusababisha uvunjaji wa amani na utulivu na kwamba hali hiyo haiwezi kuzuilika mpaka mtu huyo ambaye ni sababu ya uvunjifu huo wa amani na utulivu amekamatwa na kuwekwa kizuizini.
Chini ya kifungu cha 6 (2) na (3) mtu ambaye atakamatwa kwa amri ya Mkuu wa Mkoa ana haki ya kuelezwa sababu za kukamatwa na kuwekwa kizuizini.
Pia kwa vyovyote vile mtu huyo hatawekwa kizuizini kwa muda wa zaidi ya masaa 48 mfululizo bila kufikishwa mahakamani.
Mamlaka ya Wilaya
Kwa mujibu wa kifungu cha 4 (2) cha Sheria ya Tawala za Mikoa 1998, Rais wa Zanzibar atateua Mkuu wa Wilaya katika kila Wilaya ya Zanzibar.
Mkuu wa Wilaya atatekeleza ndani ya Mkoa wake yale majukumu ambayo Mkuu wa Mkoa anayatekeleza chini ya Sheria.
(Kifungu 6 (5) na 7 vya Sheria Namba 1 ya 1998).
Mamlaka ya Shehia
Kwa mujibu wa sheria Namba 1 ya 1998, mbali ya mamlaka ya Mikoa na wilaya limetafsiriwa kwenye kifungu cha 2 cha Sheria hii kuwa ni eneo lote ambalo hapo awali lilikuwa ni eneo la tawi la chama cha Mapinduzi au eneo jengine lolote ambalo litatengwa na mamlaka kwa ajili hiyo.
Hata hivyo haikuelezwa ni mamlaka gani yenye madaraka ya kufanya utengaji huo.
Chini ya kifungu 15 cha sheria ya tawala za Mikoa, Wakuu wa Mikoa (wakishauriwa na Wakuu wa Wilaya) ndio watawateuwa masheha.
Sheha atateuliwa miongoni mwa watu wa shehia inayohusika.
Kazi za Masheha ni:-
(i). kutekeleza Sheria, sera, amri na maelekezo yote ya serikali kwa ajili ya kuhakikisha utekelezaji wa sheria na utunzaji wa amani;
(ii). kusululisha na kutatua matatizo yote yanayojitokeza katika jamii kwa kutumia busara, desturi, silka na mila za watu wa eneo linalohusika;
(iii). kuweka kumbu kumbu kuhusu usajili wa ndoa, talaka, vizazi na vifo, vibali vya ngoma, vyeti vya kusafirishia mazao, mifugo mkaa na vyenginevyo kama itakavyoelekezwa na taasisi husika;
(iv). kudhibiti uhamiaji wa watu katika shehia yake;
(v). kupokea taarifa ya mikutano yote ya hadhara katika eneo lake; na (vi). kufanya mambo mengine yote ya halali kama ambavyo ataagizwa na Mkuu wa Wilaya yake.
Katika kutenda shughuli zake, kila sheha anao uwezo wa kumwita mtu yeyote, na endapo mtu huyo atakataa, anao uwezo wa kutoa hati ya wito ili mtu huyo afike mbele yake au atoe taarifa inayohitajiwa na Sheha.
Endapo mtu aliyepewa hati ya wito wa Sheha anakataa kwenda, Sheha anaehusika atapeleka taarifa hiyo kwenye kituo cha Polisi ambacho kitampeleka mtu huyo kwa Sheha.
Hata hivyo, mtu yeyote ambae amekataa wito wa Sheha atakuwa ametenda kosa na akipatika na hatia atatozwa faini isiyozidi Tshs. 10,000.
Kwa mujibu wa kifungu cha 17 (7), katika kazi zake Sheha atawajibika kwa Mkuu wa Wilaya yake.
Ili mtu aweze kuteuliwa kuwa Sheha ni lazima awe na sifa zifuatazo:
(i). awe Mzanzibari;
(ii). awe ni mtu mwenye kuheshimika;
(iii). awe ni mtu mwenye tabia nzuri;
(iv). awe na umri usiopungua miaka 40;
(v). awe amepata elimu ya msingi na anajua kusoma na kuandika kiswahili na/au kiingereza; na
(vi). awe ameishi kwenye shehia hiyo kwa muda usiopungua miaka 15.

No comments:

Post a Comment