Thursday, August 12, 2010

Wabunge, Wawakilishi twambieni mtafanya nini kupunguza mimba kwa wanafunzi wa kike?

SKULI za awali, msingi na sekondari sasa zimeenea kila kona ya Zanzibar.

Wazanzibari wameitikiwa kwa vitendo wito wa serikali wa kuwataka kuanzisha skuli katika maeneo yao huku serikali nayo ikiunga mkono kwa upande wake lengo ni kukidhi mahitaji ya wanafunzi hasa kutokana na kuwepo idadi kubwa ya wanafunzi wanaomaliza skuli za msingi na kuhitaji kuingia sekondari.

Sitaki kuzungumzia yote, leo hii nachagua tatizo moja tu ambalo ni wanafunzi wengi wa kike kupata ujauzito na hivyo kulazimika kukatisha masomo.

Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali (2010), kila mwaka kiasi cha wanafunzi 50 wa kike hukatisha masomo kutokana na kupewa ujauzito, hali ambayo huwafanya wanafunzi kufuta kabisa ndoto zao za kujiimarisha katika maisha yao ya baadae na kuendelea kuwa tegemezi.

Inawezekana tatizo hili limekuwa kubwa zaidi kutokana na kuachiwa walimu na wazee peke yao, huku wabunge, wawakilishi na madiwani ambao wana wajibu mkubwa wa kusimamia skuli hizi kwa mambo yote ya kulea wanafunzi wanaosoma, wakilipa kisogo tatizo hili.

Wao wamezigeuza skuli kama sehemu ya mradi wa kupata kura za wananchi wa maeneo hayo mara uchaguzi unapokaribia.

Nasema hivyo kwa vile mwanasiasa anapopata fursa ya kwenda kutembelea skuli, anapeleka tu msaada wa mabati au saruji, ili aweke kwenye orodha ya mambo aliyoyafanya wakati wa uongozi wake, lakini hawatengi muda wa kuzungumza na wanafunzi mara wanapotembelea skuli hizo.

Wengi wanakwenda kutoa msaada ilimradi waonekane wamefanya mambo mengi kusaidia skuli zilizo katika majimbo yao, wakisahau kwamba kumbe wanafunzi wanajitaji msaada mkubwa zaidi wa kupewa elimu ya kujitambua kutoka kwa viongozi wao.

Kwa bahato nzuri nimekuwa nikipata fursa ya kuzungumza na baadhi ya wanafunzi na kuwauliza kama wamewahi angalau kukaa na Wawakilishi wao, Wabunge au Madiwani kuzungumzia matatizo yao, wengi walikiri kuwa hawajawahi.

Wanafunzi wengine hawafahamu hata majina ya wabunge, wawakilishi na madiwani wao na wengine hata sura zao.

Hii ni ishara kuwa licha ya wanasiasa kudai kuwa wanatembelea skuli zao; lakini hawatoi fursa ya kuzungumza na wanafunzi.

Hali hii imefanya hata ukizungumza na wabunge, wawakilishi na madiwani licha ya kujigamba kutembelea skuli hizo, lakini hawana takwimu sahihi za idadi ya wanafunzi wanaoacha shule kwa sababu ya ujauzito.

Kinakera zaidi i kwa diwani ambaye anashughulika na skuli moja pengine kwenye wadi yake, naye hana takwimu za wanafunzi wanaokatisha masomo kwa tatizo la mimba katika skuli yake.

Hii ni kwa sababu diwani akienda kwenye skuli jambo la maana analoona ni kusimamia ujenzi wa nyumba ya mwalimu au kuangalia ujenzi wa vyumba vya madarasa na kama wazazi wametoa mchango kwa ajili ya ujenzi wa darasa au nyumba ya mwalimu.

Hii ni kazi nzuri wanayofanya wanasiasa wetu majimboni, lakini kinachochefua ni kuona viongozi hawa ambao tumewapa dhamana ya kutuongoza, wanaonekana hawajali tatizo la wanafunzi ambao wanakatisha masomo kwa ujauzito.


Hii ina maana kuwa kitendo cha viongozi hawa wa kisiasa kutokerwa na tatizo hili la wanafunzi kupata ujauzito, ndicho kinachofanya wasisumbuke kuzungumzia suala hilo.

Tabia hii ya wanasiasa wetu kutofanya suala la mimba kuwa ajenda yao ya kisiasa, limefanya tatizo hili kuongezeka na iwapo hali hii ikiachwa iendelee, wanafunzi wengi wa kike wanaofaulu hawatamaliza masomo yao.

Ni wakati muafaka sasa, kwamba suala hili liwe ajenda ya wanasiasa, wayaone matatizo mengi yanayowafanya wanafunzi hawa wapate ujauzito ili waweze kuyashughulikia.

Bila kufanya hivyo matatizo yanayochangia wanafunzi hao kupata ujauzito, yataendelea kuwepo na idadi ya wanaopata ujauzito itaongezeka.

Naomba wagombea watakaopitishwa na vyama vyao kugombea, Ubunge, Uwakilishi na Udiwani waliingize kwenye ajenda suala hili ili kuokoa watoto hawa wa kike wasikatishe masomo.

Watwambie wakati wa kampeni watafanya nini kupunguza au kulimaliza tatizo hili linalozikabili skuli nyingi za kata.
Ingawa kwa upande wake serikali kuu, imechukua juhudi za makusudi kuhakikisha wanafunzi wanaokatisha masomo kwa ujauzito wanarejea skuli baada ya kujifungua, utekelezaji wa sera hii mihimu kuwekewa msisitizo ili kuhakikishwa wanafunzi wa kike wanapata fursa sawa ya elimu na wanaume.

Tunaamini kwa pamoja tunaweza kuliweka tatizo la mimba kwa wanafunzi kuwa ajenda muhimu kwa jamii yetu.

Michango, misaada kwa wagombea na vyama vya siasa isitolewe wakati wa kampeni

Taarifa ya gharama itakayotolewa na mgombea, kwa madhumuni ya sheria hii, na pasipokuwa na sababu nyegine itachukuliwa kuwa ni ushahidi unaotosha kuwa mgombea amewasilisha taarifa ya fedha kwa Katibu wa Chama wa Wilaya au Katibu Mkuu atatoa hati ya uthibitisho kuwa mgombea huyo ametekeleza sheria.

Kwa kuzingatia umuhimu wa shreia hii, michango ya hiyari na zawadi zinazotolewa kwa chama na wagombea inataka pawepo na uwazi katika utoaji wake.

Sheria inaeleza kwamba kila chama cha siasa kilichopokea michango inayozidi shilingi milioni moja kutoka kwa mchangiaji binafsi au shilingi milioni mbili kutoka kwa taasisi kitoe taarifa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa kwa kujaza fomu maalum.

Sheria pia inataka fedha hizo zihifadhiwe katika hesabu ya benki (account) maalum itakayofunguliwa kwa ajili hiyo.

Fedha hizo zitalipwa na kutumika kutoka account hiyo, kama ilivyoelezwa na sheria hii katika kifungu cha 11(1).

Sheria pia inafafanua utaratibu wa vyama au wagombea kupata misaada kutoka nje ya nchi.

Sheria inazuia michango na misaada hiyo isitolewe wakati wa kampeni.

Inaruhusu Vyama vya Siasa au wagombea kupokea misaada kutoka nje ya nchi siku tisini (90) kabla ya uchaguzi mkuu au siku thelathini (30) kabla ya uchaguzi mdogo.

Pia inataka kuwepo uwazi na taarifa itolewe kwa Msajili wa Vyama vya Siasa.

Uwajibikaji wa Asasi zisizo za Kiserikali

Sheria hii inaweka pia sharti la uwajibikaji kwa taasisi zisizo za kiserikali, vikundi vya kidini au vikundi vya kijamii ambavyo, kwa madhumuni ya uchaguzi vingependa kushiriki kwa:

(a) Uhamasishaji au

(b) Kuelimisha jamii katika mwenendo wa kampeni za uchaguzi. Vikundi hivi vinatakiwa kutoa taarifa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa kuhusu gharama zilizotumika katika uchaguzi ndani ya siku tisini (90) baada ya uchaguzi.

Pia sheria inaeleza kuwa taasisi hizi au vikundi vya kijamii hivyo, havitaruhusiwa kutumia gharama zaidi ya kiwango kilichoanishwa katika kanuni.

Hivyo basi taasisi za kiraia, taasisi za kidini au taasisi za kijamii itakayaohusika katika kuchangia shughuli za uchaguzi inayo wajibu wa kutunza taarifa za fedha zinazoelezea mapato na matumizi hayo.

Viwango vya gharama za uchaguzi

Sheria ya gharama za uchaguzi inaweka utaratibu wa kudhibiti gharama za uchaguzi kwa kumpa mamlaka Waziri mwenye dhamana kuweka viwango vya gharama za uchaguzi.

Viwango hivyo vimezingatia, tofauti ya majimbo, idadi ya watu, aina ya wagombea pamoja na miundombinu.

Kwa mfano, kwa wagombea Ubunge kiwango cha chini ni milioni 30, wakati kiwango cha juu ni milioni 80 na viti maalum isioyozidini shilingi milioni 10.

Hivyo basi chama au mgombea atakayevuka kiwango kilichowekwa lazima atoe maelezo ya kuridhisha bila kufanya hivyo atakuwa ametenda kosa.

Lengo ni kujenga nidhamu na usawa miongoni mwa vyama vya siasa na wagombea katika uchaguzi.

Mgawanyo wa matumizi baina ya Chama na mgombea

Sheria ya gharama za uchaguzi katika kifungu cha 17(1) kinaruhusu mgawanyo wa gharama za uchaguzi zilizotumika na mgombea mwenyewe na zile ambazo chama cha siasa kimetumia kumtangaza mgombea pamoja na mikutano yote; kwa hali hiyo chama kitafanya mambo yafuatayo.

a) Kuweka mgawanyo ulio wazi baina ya matumizi ya mgombea kadiri itakavyowezekana na yale yaliyoyofanywa na chama.

b) Ndani ya siku 30 baada ya kupiga kura chama kitamfahamisha mgombea kiasi cha gharama kilichogawanywa ambacho kitakuwa ni sehemu ya gharama za uchaguzi za mgombea.

Wednesday, July 28, 2010

Mgombea anaweza kutumia gharama zake mwenyewe wakati wa kampeni

Na Juma Khamis

KWA muda mrefu, Tanzania haikuwa na mfumo maalum wa kusimamia na kuratibu gharama za uchaguzi kwa gombea wa vyama vya siasa.

Katika uchaguzi wa mwaka 2010, kumekuwepo na mawazo na pia kujengeka utamaduni kwamba uongozi unaweza kununuliwa kwa fedha.

Tofauti za uwezo wa wagombea zimekuwa kubwa kiasi ambacho wananchi hawapati fursa ya kuchagua viongozi wanaowataka badala yake wale wenye fedha tu ndio wanachaguliwa kwa sababu ya fedha zao.

Baada ya kuona hali hiyo, serikali ya Tanzania iliona iko haja ya kuimarisha demokrasia ya uchaguzi kwa kuhakikisha kwamba kunakuwepo mazingira yaliyo salama na sawa kwa wagombea wakati wa uchaguzi ili kuweza kupata viongozi wenye uwezo wa kuongoza na kuwatumikia wananchi kwa ushawishi wa sera ya vyama vyao na sio fedha.

Katika kutimiza dhamira hiyo, serikali iliamua kutunga sheria ya gharama za uchaguzi namba 6 ya mwaka 2010 iliyopitishwa na Bunge Februari 11, 2010.

Hata hivyo, kwa kuwa sheria hii bado haijarasimishwa na Baraza la Wawakilishi kutumika katika mamlaka ya Zanzibar, haitakuwa na meno ya kuuma (haitafanya kazi) kwa nafasi za Urais wa Zanzibar, Uwakilishi na Udiwani, badala yake itatumika kwa nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Bunge (ingawa sheria ya uchaguzi kwa Wabunge wa Zanzibar inasimamiwa na sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar nambari 11 ya mwaka 1984).

Lengo la sheria hii ni kuutambua kisheria mchakato wa uteuzi wa wagombea ndani ya vyama vya siasa kuanzia ngazi ya kura za maoni na kusimamisha wagombea.

Kuweka utaratibu wa kisheria utakaosimamia na kuratibu mapato na kudhibiti matumizi pamoja na gharama za uchaguzi kwa vyama vya siasa na wagombea.

Kuweka viwango kwa matumizi na gharama za uchaguzi; kuweka utaratibu utakaosimamia mapato na matumizi ya vyama vya siasa ikiwa ni pamoja na zawadi, misaada na michango itakayotolewa na wagombea au wahisani wakati wa kampeni za uchaguzi.

Kudhibiti michango na zawadi kutoka nje, kuweka utaraibu na mfumo wa uwajibikaji wa mapato na matumizi ya fedha za uchaguzi kwa upande wa vyama vya siasa na wagombea na kuainisha adhabu kwa watakaokiuka masharti yaliyowekwa na sheria yenyewe.


Nini gharama za uchaguzi?

Gharama za uchaguzi maana yake ni fedha zote ambazo zimetumika au gharama zote zilizotumika kwa ajili ya kuendesha au kusimamia kura za maoni, kampeni za uchaguzi na uchaguzi kwa chama cha siasa, mgombea na serikali. Hii imeelezwa kwa kina katika kifungu cha 7(1) cha sheria ya gharama za uchaguzi.

Kwa hivyo, gharama ni matumizi yote yatakayohusika wakati wa kura za maoni ambayo yatakuwa yamegharamiwa na chama cha siasa, matumizi au gharama zozote zitakazo husika na chama ili kuwezesha uteuzi wa mgombea wake, gharama zozote au matumizi yoyote yatakayohusika na chama cha siasa au mgombea wakati wa kampeni ikiwa ni pamoja na gharama zote zitakazotumika kwa ajili ya vikundi vya uhamasishaji kwa ajili ya kumnadi mgombea.

Pia gharama za chakula, vinywaji, malazi au usafiri ambazo mgombea amegharamia wakati wa kampeni na gharama zozote au matumizi yoyote yatakayohusika na serikali, chama cha siasa au mgombea wakati wa uchaguzi yatajumuisha gharama za uchaguzi.

Sheria imeweka bayana kwamba kila chama cha siasa kitagharamia kampeni za uchaguzi kwa kutumia gharama za uchaguzi zinazotokana na vyanzo vyake, kwa mujibu wa kifungu cha 8(1) cha sheria hii.

Hata hivyo, kifungu cha 8(2) kimezingatia kuwa mgombea anaweza kutumia gharama zake mwenyewe wakati wa kampeni pale inapobidi kulingana na mahitaji ya kampeni zake.

Uwazi wa mapato na matumizi

Sheria hii inaweka sharti la uwazi katika mapato na matumizi ya vyama na wagombea kwa ajili ya uchaguzi kabla, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi.

Sheria hii pia inaelekeza utaratibu wa kufuatwa na vyama vya siasa na wagombea kutoa taarifa zao za mapato na matumizi ya uchaguzi, kama ilivyobainishwa katika kifungu cha 9(1) ambacho kinasema
“Mgombea atatakiwa kutoa taarifa ya fedha alizonazo na anazotarajia kupata na anakusudia kuzitumia kama gharama za uchaguzi ndani ya siku saba (7) baada ya siku ya uteuzi.”

Taarifa hizo zitawasiliskwa kwa Katibu Mkuu wa chama kwa mgombea wa nafasi ya Urais na kwa mgombea wa nafasi ya Ubunge taarifa zake ataziwasilisha kwa Katibu wa Chama wilaya.

Kila chama cha siasa kinachoshiriki katika uchaguzi ni lazima ndani ya siku thelathini (30) baada ya siku ya uteuzi wa wagombea kufanywa na Tume ya Uchaguzi kitoe taarifa kwa Msajili juu ya fedha zote ambazo kinakusudia kutumia kama gharama za uchaguzi; na kutumia kwa kuwadhamini wagombea wa chama hicho zikiwa ni kama gharama za uchaguzi.

Kanali Farrah atumia 99m/- kuimarisha chama, maendeleo ya jimbo Rahaleo

UPIGAJI kura ya maoni kwa wagombea Ubunge na Uwakilishi kwa tiketi ya CCM, itafanyika Agosti 1, siku moja tu baada ya Wazanzibari kupiga kura ya maoni kuhusu mfumo mpya wa serikali.

Kura hiyo inafanyika huku majimbo yakiwa yamefurika wagombea, hali ambayo haijawahi kutokea katika historia ya chama hicho.

Wagombea wa zamani wamekuwa wakijaribu bahati zao kwa mara nyengine tena huku wapya nao wakitaka kuingia kwa mara ya kwanza.

Miongoni mwao yumo Kanali mstaafu wa Jeshi, Saleh Ali Farrah, anaegombea tena nafasi ya Ubunge katika jimbo la Rahaleo.

Kanali Farrah anawania nafasi hiyo akiwa na matarajio makubwa ya kushinda, hasa kutoka na juhudi zake kubwa alizochukua katika kulijenga kimaendeleo jimbo la Rahaleo pamoja na chama cha Mapindunzi kwa ujumla.

Farah anasema, amefanya mengi ya kujivunia na ya kupigiwa mfano kwa wananchi wa Rahaleo, akisema maendeleo yaliyofikiwa hayajawahi kuonekana katika miaka kadhaa iliyopita.

Kanali Farrah anasema katika kipindi chake cha miaka mitano cha kuwatumikia wananchi wa Rahaleo, ametumia jumla ya shilingi milioni 99 kwa ajili ya kuleta maendeleo ya jamii, elimu, afya, michezo na kuimarisha shughuli za chama.

Farrah katika kipindi chake kilichomalizika pamoja na mambo mengine, ameweza kulipa posho kwa watendaji wa chama kila mwezi kati ya shilingi 10,000 na 30,000 kwa ngazi ya matawi, wadi na jimbo.

Malipo hayo ameyafanya katika kipindi cha miezi 56, ambayo yamemugharimu shilingi milioni 13,440,000.

Katika michango ya kuimarisha chama, Farrah kila mwezi amekuwa akitoa mchango wa shilingi 70,000 makao makuu ya CCM Kisiwandui, ambapo kwa Mkoa wa Mjini Magharibi amekuwa akichangia shilingi 40,000 wakati kwa wilaya ya mjini amekuwa akichangia shilingi 20,000 na kufanya jumla ya pesa alizochangia katika kipindi cha miezi 56 kufikia milioni 7,280,000.

Hakuishia hapo, kwa upande wa matembezi ya mshikamano, Kanali Farrah amechangia kila mwaka shilingi 200,000 na kufanya idadi ya fedha alizochangia katika matembezi hayo kufikia shilingi 1,000,000.

Katika uimarishaji wa maskani kaka ya Kisonge, Kanali Farrah amechangia shilingi 1,000,000 kwa maskani hiyo na kiasi kama hicho kwa maskani ya Kachorora ambazo ni maskani zenye nguvu kwa Zanzibar.

Akizungumzia uimarishaji wa wadi na jimbo, Farrah alisema amechangia mashine ya fotokopi kwa kila wadi ya jimbo hilo, huku Wadi ya Rahaleo ambao ina matawi matatu ikipatiwa shilingi 2,000,000 wakati Wadi ya Mlandege ambayo ina matawi manne akichangia shilingi 4,000,000.

Kanali Farrah, amekwenda mbali zaidi hata nje ya jimbo lake, anasema katika kufanikisha uchanguzi mdogo wa Magogoni, alichangia shilingi 1,000,000 wakati katika mfuko wa Mkoa wa kufanikisha uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 tayari ameshachangia shilingi 5,000,000 huku mfuko wa wilaya akichangia shilingi 1,500,000.

Katika matengenezo ya matawil ya Mwembeshauri, Rahaleo na tawi la Makadara, Kanali Farrah amechangia shilingi 9,750,000 huku katika daftari la kudumu la wapiga kura awamu ya kwanza, mwanajeshi huyo wa zamani alichangia shilingi 1,500,000 na awamu ya pili kiasi kama hicho cha fedha na kufanya idadi ya pesa alizochangia kufikia shilingi 3,000,000.

Ili jamii iweze kupata elimu bora, Kanali Farrah pia hakuwa nyuma akiamini kama kiongozi wa jimbo la Rahaleo huo ni wajibu wake.

Katika suala hilo, amechangia jumla ya shilingi 10,120,000 ikiwa ni pamoja mchango kwa wanafunzi wa michepuo wa skuli zilizomo ndani ya jimbo lake, tunzo kwa walimu, uchimbaji wa kisima kwa ajili ya wanafunzi na kumalizia ujenzi wa skuli ya msingi ya makadara.

Kwa kuwa Farrah pia ni mwanamichezo, muda wake mwingi amekuwa akiitumia kwa hali na mali kusaidia wanamichezo.

Tayari ametoa jezi seti moja yenye thamani ya shilingi 450,000 kwa klabu ya Mwembeshauri na klabu ya Rangers ya Makadara ambayo ilikabidhiwa seti ya jezi yenye thamani ya shilingi 250,000.

Aidha ametoa seti tatu za jezi kwa timu ya Jimbo na huduma nyengine kwa timu hiyo zenye thamani ya shilingi 4,500,000.

Mbali ya juhudi hizo alizochukua, pia amekuwa mstari wa mbele katika kukabiliana na tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama.

Katika nyanja hiyo, amechipa visima viwili katika Wadi ya Rahaleo kilichogharimu shilingi 3,000,000 na chengine Mwembeshauri ambacho kimegharimu shilingi 3,000,000.

Visima hivyo vyote vinatoa huduma kwa wananchi wa maeneo hayo kwa wakati wote.

Farrah pia amekiwa akiumwa na tatizo kwa watu wenye ulemavu; tayari amenunua viti vya walemavu kwa gharama ya shilingi 17,500,000 kuwasaidia wananchi ndani ya jimbo lake.

Katika kuvisaidia vikundi vilivyoanzishwa katika jimbo lake, Mbunge huyo anaemaliza muda wake ametumia wastani wa shilingi 1,500,000 kwa vikundi 15 kufungua vitabu vya benki ili kuweza kuendeleza shughuli zake.

Kwa watu wenye matatizo binafisi, Farrah ametumia shilingi 17,340,000 na anaamini bila ya msaada wao kumchagua katika uchaguzi wa mwaka 2005 asingeweza kutekeleza hayo.

Kanali Farrah anasema anarejea tena kuomba ridhaa ya wananchi jimboni akiwa msafi na akiamini kwamba amekamilisha yale ambayo wananchi walitaka ayatekeleze.

Farrah amewahakikishia wananchi wa Rahaleo kwamba, endapo watamchagulia tena watarajie maendeleo mapya ambayo yatakidhi mfumo wa sasa wa ilimwengu.

Farrah alizaliwa Juni 5, 1949 na kuanza elimu ya msingi katika skuli ya St Joseph Convent mwaka 1958 na kuhitimu mwaka 1965.

Baadae alijiunga na skuli ya Lumumba kuanzia mwaka 1966 hadi mwaka 1969 kabla ya kujiunga na chuo cha kijeshi mwaka 1980 hadi mwaka 1981.

Katika utumishi Farrah amelitumikia Jeshi la Wananchi wa Tanzania katika ngazi mbali mbali kuanzia mwaka 1971 hadi mwaka 1990 alipoteuliwa kuwa mlinzi wa Rais wa Zanzibar hadi mwaka 1999.

Katika kukitumikia chama alijiunga na ASP mwaka 1972, mbapo mwaka 1975 alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa tawi la ASP hadi mwaka 1976.

Mwaka 1977 alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa CCM hadi mwaka 1989.

Wednesday, July 21, 2010

Wagombea, mawakala wanayo haki ya kuhoji na kuangalia hatua za kujumlisha kura

Kuhesabu kura ni hatua inayofuata mara baada ya zoezi la kupiga kura kumalizika. Sheria ya uchaguzi imeweka utaratibu wa kuhesabu kura katika vituo vya kupigia kura.

Kwa kifupi, wasimamizi wa vituo vya kupigia kura ndio watakaohusika na kuhesabu kura vituoni.

Wakati wa kuhesabu vituo vya kupigia kura na maofisa wa kupiga kura, vitaitwa vituo vya kuhesabu kura na maofisa nao watakuwa maofisa wa kuhesabu kura.

Watu walioruhusiwa kuwemo katika vituo vya kupigia kura ndio watakaoruhusiwa kuwemo katika vituo vya kuhesabu kura.

Kifungu cha 80 cha sheria ya uchaguzi kimeweka utaratibu mzuri wa namna ya kuhesabu kura.

Lakini kabla ya kuhesabu kura msimamizi wa wa kituo atatakiwa kutoa taarifa zifuatazo kwa watu wanaoshikiri katika zoezi hilo.
Hesabu ya kura zilizopelekwa katika kituo cha kupigia kura
Hesabu za watu waliopiga kura
Hesabu ya kura zilizobakia ambazo hazikupigwa
Hesabu ya karatasi za kura
Idadi ya wapiga kura waliopiga kura, na
Hesabu za kura zote zilizotumika.

Na baada ya hapo, atakagua kifungio na kuhakikisha kuwa hakikufunguliwa au kufanyiwa udanganyifu, kufungua kifungio na kufungua sanduku tayari kwa kauanza kuhesabu kura.

Hatua hizi ni lazima zifuatwe ili kutekeleza yale matakwa ya kanuni na kisheria inayosema kwamba ‘sio tu kwamba haki itendeke bali ionekane bayana ikitendeka’.

Sheria inaelezea uwazi zaidi wa kuhesabu kura, kwa kumtaka msimamizi wa kuhesabu kura kukunjua karatasi ya kura na kutamka kwa sauti kilichoonekana katika karatasi hiyo, na hayo lazima yashuhudiwe na watu waliopo katika kituo cha kuhesabu kura.

Hata hivyo, ili kujua ipi halali na ipi batili, jukumu hilo limewekwa kwa Tume kwa kutunga kanuni kueleza ni ipi kura halali na ipi sio halali.

Hata hivyo, utaratibu unaotumika sasa ni kukubaliana kwa waliopo katika chumba cha kuhesabu kura, ipi kura halali na ipi kura batili.

Kujumlisha kura

Hii ni hatua inayofuata baada ya kuhesabu kura kutoka vituoni.

Ni hatua ambayo matokeo yote ya vituo vya kupigia kura hujumlishwa katika jimbo la uchaguzi ili kupata matokeo ya jumla kwa jimbo zima na hatimae kumpata mshindi.

Kifungu cha 83A kimewataja watu wanaoruhusiwa kuwepo wakati wa zoezi la kujumlisha matokeo ni.

(a) Msimamizi wa uchaguzi
(b) Msaidizi Msimamizi wa uchaguzi
(c) Mjumbe wa Tume
(d) Mkurugenzi wa Uchaguzi au Afisa wa uchaguzi wa Tume
(e) Mgombea
(f) Wakala wa kuhesabu kura
(g) Polisi au mtu mwenye jukumu la kuweka usalama katika kituo cha kuhesabu kura
(h) Waangalizi walioruhusiwa na Tume.

Wakati wa zoezi la kujumlisha matokeo, wagombea au wakala wao wanayo haki ya kuhoji na kuangalia hatua zote za kujumlisha kura na iwapo watakuwa na mashaka wanaweza kuomba kwa msimamizi wa uchaguzi ili kujiridhisha na ujumlishaji huo.

Aidha kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi, matokeo ya kura ya Urais yatajumlishwa na tofauti na yale ya Wawakilishi na Udiwani.

Kutangaza matokeo

Kutangaza matokeo ya uchaguzi ni hatua ya mwisho katika uchaguzi kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi.

Mamlaka ya kutangaza matokeo ya uchaguzi kwa ngazi zote yapo kwa Tume.

Kwa mujibu wa kifungu cha 88, inaelezwa kuwa, mara baada ya zoezi la kuhesabu na kujumlisha kura kukamilika na matokeo kuthibitishwa, Msimamizi wa uchaguzi atamtangaza mgombea aliyepata wingi wa kura halali.

Taarifa za matokeo pia zitapelekwa kwa maandishi kwa mshindi na baadae kutangazwa katika Gazeti rasmi la serikali.
Aidha kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi matokeo ya uchaguzi kwa uwakilishi na udiwani yatatangazwa na Wasimamizi wa uchaguzi wa Majimbo vituoni, na kwa ngazi ya Urais yatatangazwana Tume makao makuu.

Kwa maana hiyo, matokeo halali kwa mujibu wa sheria ni yale yatakayotangazwa na Tume na sio vyenginevyo.

Hizi ndizo taratibu za uchaguzi wa viongozi wa Zanzibar chini ya Sheria ya Uchaguzi Nam 11 ya mwaka 1984.

Thursday, July 15, 2010

Kampeni ya nyumba kwa nyumba ni kosa kwa mujibu wa sheria

Uteuzi wa wagombea wa udiwani

Ama kwa upande wa wagombea wa udiwani, masharti ya uteuzi yameelezwa katika kifungu cha 59 na 60, masharti yenyewe ni kama yafuatayo:

(a) Mgombea lazima awe amedhaminiwa na chama cha siasa kilichosajiliwa.

(b) Mgombea lazima awe amedhaminiwa kwa maandishi na wapiga kura wasiopungua kumi na tano (15) walioandikishwa kuwa wapiga kura katika eneo la uchaguzi analogombea.

(c) Mgombea alipe dhamana ya kima cha fedha kama kitakachowekwa na Tume.

Kama ilivyo kwa uteuzi wa wagombea wa urais, kwa upande wa uwakilishi na udiwani, baada ya hatua za chama au mgombea kuwasilisha fomu zao za kugombea kwa Tume, Tume itafanya uhakiki wa sifa na masharti mengine kama yalivyoelezwa na Katiba na Sheria ya uchaguzi, na baadae itafanya uteuzi wa wagombea waliotimiza sifa na vigenzo vilivyowekwa na katiba pamoja na sheria.

Kufanya kampeni
Kampeni ni hatua inayofuata baada ya uteuzi wa wagombea. Kwa kawaida kampeni hufanywa na chama au mgombea wa chama.

Hivyo sheria ya uchaguzi imeweka masharti ya kufuatwa na vyama au wagombea wakati wa kufanya kampeni kwa ajili ya uchaguzi.

Kifungu cha 56 kinaelezea kuwa kila chama kitawasilisha kwa Tume ya Uchaguzi ratiba ya mikutano ya kampeni inayoonesha wakati na pahali mikutano hiyo itakapofanyika na nakala ya ratiba hiyo kupelekwa kwa Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa wa Jeshi la Polisi kwa ajili ya kuandaa usalama wakati wa kampeni.

Tume inatakiwa kuhakikisha kuwa ratiba ya kampeni ya chama kimoja haigongani na ratiba ya chama chengine ili kuondoa hali ya kuwepo kwa kampeni mbili katika sehemu moja.

Sharti jengine lililowekwa katika kifungu hichi ni kwamba chama au mgombea kutofanya kampeni katika maeneo ya ibada au taasisi za taaluma.

Hata hivyo, maeneo ya taalamu au taasisi za ibada zimeelezwa kuwa ni maeneo yote yanayotumiwa na waumini kufanyia ibada ikiwemo misikiti, makanisa au madrasa au sehemu nyingine yoyote inayotumiwa na waumini kwa ajili ya ibada.

Aidha taasisi za taaluma ni sehemu yoyote inayotumika kwa ajili ya kutoa taaluma ikiwa ni pamoja na shule, vyuo na maeneo kwa hayo.

Pia sheria imepiga marufuku kufanya kampeni za nyumba kwa nyumba.

Kampeni za nyumba kwa nyumba ni kwa chama au mgombea kupita majumbani na kutangaza au kushawishi watu wapige kura chama au mgombea fulani.

Kupiga kura

Baada ya hatua ya kampeni kumalizika, hatua inayofuata ni kupiga kura. Sheria ya uchaguzi inasema kuwa Tume itatangaza siku ya kupiga kura na namna ya kupiga kura.

Zoezi la kupiga kura litafanyika katika vituo vya kupigia kura ambapo wapiga kura watatakiwa kufuata maelekezo yatakayotolewa na Tume juu ya utaratibu na namna ya kupiga kura, ikiwemo jinsi ya kujipanga kwa utaratibu maalum kama utakavyowekwa na kutangaza na Tume.

Hata hivyo, kupiga kura itakuwa kwa wale walioandikishwa na kupewa shahada za kupigia kura.

Kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi kila mtu atatakiwa apiga kura katika sehemu aliyoandilishwa kama mpiga kura katika eneo hilo, kinyume na hivyo mtu hatokuwa na haki ya kupiga kura.

Kuwepo utaratibu wa kuwawezesha wapiga kura wapige kura zao kwa njia ya siri na kwa upande wa wale watu wasioona, walemavu wa viungo au kushindwa kusoma, Tume ya uchaguzi inatakiwa kuanda utaratibu wa kuwawezesha watu wote hao wapige kura kwa namna iliyo huru, ikiwemo kuwaruhusu watu wao karibu kuweza kuwasaidia kupiga kura zao.

Vile vile sheria inaelekeza kuwa katika vituo vya kupigia kura, kutaruhusiwa watu maalum kuingia au kuwepo katika vituo hivyo. Watu watakaoruhusiwa kuwemo katika kituo cha kupigia kura ni:

(i) Mkuu wa kituo cha kupigia kura;
(ii) Msaidizi wa kituo cha kupigia kura
(iii) Wakala wa upigaji kura
(iv) Mpiga kura
(v) Mtu anayemsaidia mpiga kura mwenyewe ulemavu
(vi) Mwangalizi wa uchaguzi aliyepewa utambulisho na Tume
(vii) Mgombea
(viii) Mjumbe wa Tume
(ix) Mkurugenzi wa uchaguzi
(x) Afisa wa uchaguzi
(xi) Afisa wa polisi au mtu mwengine mwenye dhamana ya usalama katika kituo cha kupigia kura; na
(xii) Msimamizi wa uchaguzi na Msimamizi Msaidizi wa uchaguzi.

Hivyo kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi hawa ndio watu wanaoruhusiwa kuingia katika kituo cha kupigia kura.

Aidha mara baada ya zoezi la kupiga kura kumalizika, sheria inaelekeza utaratibu wa kuhidafhi masanduku ya kura baada ya kukubaliana na wahusika wote na kuyafunga namna ambavyo hayataweza kufunguliwa na hakuna chochote kinachoweza kuingizwa katika masanduku hayo.

Kuhesabu kura

Kuhesabu kura ni hatua inayofuata mara baada ya zoezi la kupiga kura kumalizika. Sheria ya uchaguzi imeweka utaratibu wa kuhesabu kura katika vituo vya kupigia kura.

Kwa kifupi, wasimamizi wa vituo vya kupigia kura ndio watakaohusika na kuhesabu kura vituoni.

Wakati wa kuhesabu vituo vya kupigia kura na maofisa wa kupiga kura, vitaitwa vituo vya kuhesabu kura na maofisa nao watakuwa maofisa wa kuhesabu kura.

Sunday, July 4, 2010

Dk. Shein: Msiwachague viongozi wachoyo, wabinafsi, wasiopenda umoja

WATANZANIA wametakiwa kuwa macho katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu na kuacha kuwachagua viongozi, wabinafsi, wachoyo na wanaopinga umoja nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Ali Mohammed Shein, alipozindua mbio za mwenge wa Uhuru mwaka huu kitaifa, uwanja wa Kwaraa, Mjini Babati Mkoani Manyara.

“ Msiwachague viongozi wachoyo, wenye ubinafsi kwa kuweka maslahi yao mbele, na hasa wale wenye kuwagawa wananchi na kudhoofisha umoja wa Taifa”Alisema Dk. Shein.

Aidha ametoa wito kwa vyama vya siasa na taasisi za kiraia, kushajiisha wananchi kujitokeza katika kupiga kura kwenye uchaguzi uliopangwa kufanyika nchini kote Oktoba mwaka huu.

“Uchaguzi huu utatoa fursa kwa wananchi kuchagua viongozi wenye uwezo wa kuleta maendeleo nchini na kudumisha umoja, amani na utulivu bila kuzingatia ukabila, rangi, dini, mitazamo yao kisiasa au jinsia zao” alifafanua Makamu wa Rais.

Akizungumzia rushwa katika uchaguzi mkuu, Dk. Shein alieleza kuwa lengo la kupambana na vitendo hivyo la Serikali ya awamu ya nne, linaendelea, ambapo amezitaka taasisi zote zinazohusika kwa njia moja au nyengine kwenye uchaguzi huo kuwajibika ipasavyo.

Pia Dk. Shein aliwasisitiza wananchi kuongeza nguvu ya kupambana na maradhi ya malaria, Ukimwi na dawa za kulevya, pamoja na kuacha na kulaani mauaji ya albino na kuwataja wahusika wa vitendo hivyo.

Aidha Dk. Shein, alieleza mkakati wa Serikali kuwapa kipaumbele watu walio katika makundi maalum, wakiwemo wenye ulemavu, wanawake, vijana na watoto kwa kuwawezesha, ili waweze kukabiliana na matatizo yanayowakabili.

Kwa mujibu wa waziri wa Kazi na Maendeleo ya Vijana, Prof. Juma Kapuya, mwenge wa uhuru mwaka huu utamaliza mbio zake Oktoba 14, Mkoani Kigoma.

Ujumbe wa Uhuru mwaka huu ni mapambano dhidi ya malaria, dawa za kulevya, Ukimwi na uchaguzi mkuu wa amani 2010.

Hata hivyo alisema pia mwenge huo mwaka huu utaendelea kukumbusha vita dhidi ya mauaji ya albino, rushwa na mambo yenye kuhusiana na haki za wanawake.

Sherehe hizo na uzinduzi pia zimehudhuriwa na Waziri wa Kazi, Maendeleo ya Vijana, Wanawake na Watoto Zanzibar, Asha Abdalla Juma, Waziri Mkuu Mstaafu, Fredrick Sumaye, Mkurugenzi wa ILO, wabunge na viongozi wengine wa vyama vya siasa na Serikali.
Mwenge huo mwaka huu utakimbizwa na vijana sita, wawili kutoka Zanzibar na wanne Tanzania Bara, ambapo kiongozi wao ni Nassor Ali Matuzya kutoka Mkoa wa Dar es Salaam.

Raza aota maisha bora kwa Mzanzibari

Juma Khamis
KADA wa CCM Mohammed Raza amesema maisha bora kwa Mzanzibari yanawezekana na ni jambo lisilo na mjadala.

Aidha alisema suala la Muungano halitahitaji tena kuzungumza na kamati, bali itakuwa ajenda kuu ambayo itazungumzwa na viongozi wa juu wa nchi na kusisitiza kwamba kasoro zilizopo sasa zitakuwa historia tu.

Alisema kulelewa kwake ikulu kumempa nafasi ya kufahamu mambo mengi na kwamba kama atateuliwa na kuwa Rais ataongoza kasi zaidi katika sekta ya elimu na uchumi.

Alikipongeza chama cha Mapindunzi kwa kuimarisha misingi ya demokrasia na utawala bora bila bila ubaguzi wa randi, dini au ukabila.

Balozi Karume asema hana tatizo na serikali ya Umoja wa Kitaifa

Na Juma Khamis

BALOZI wa Tanzania nchini Italia, Ali Abeid Karume (60), amesema kura yake ya NDIO au HAPANA katika kura ya maoni kuamua mfumo wa uendeshaji serikali, itategemea nani atapitishwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) Julai 9 kuwa mgombea Urais wa Zanzibar katika uchaguzi mkuu ujao.

Kura ya maoni kuhusu mfumo wa serikali itafanyika Julai 31, takribani siku 20 baada ya CCM kuchagua mgombea wake wa Urais.

Balozi Karume aliyasema hayo hoteli ya Serena alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kuchukua fomu ya kuomba ridhaa kutoka chama chake kuteuliwa kuwa mgombea Urais wa Zanzibar.

“Tufikirie kwa makini kabisa kuunda serikali ya Umoja wa Kitaifa na mimi hili naliunga mkono lakini kura yangu ya NDIO au HAPANA itategemea mgombea wa Urais wa CCM atatoka upande upi,” alisema Karume.

Hata hivyo, alisema ni matarajio yake kwamba CC itawatendea haki wagombea wote na kuchagua mwanachama ‘asilia’ wa Zanzibar kugombea nafasi ya Urais wa Zanzibar.

“Tutashinda tukichagua kiongozi bora na si bora kiongozi,” alisema Balozi Karume huku akisisitiza kuwa kama atapitishwa na kushinda basi wala rushwa wataendelea tu kubakia na utaifa wa Zanzibar lakini wajiandae kutafuta nchi yao ya kuishi, akimaanisha kwamba atakabiliana kwa nguvu zake zote na mafisadi.

Akizungumzia nia yake ya kugombea kuteuliwa katika nafasi ya Urais, Balozi Karume ambae ni mdogo wa Rais wa sasa wa Zanzibar Amani Abeid Karume alisema: “Nimechangia vya kutosha Tanzania na sasa muda umefika kuchangia nchini kwangu. Nia ninayo, sababu ninayo na uwezo ninao, nakiomba chama kinipitishe.”

Balozi Karume ambae ana kadi ya CCM No. AA 270259 aliyoipata Februari 5, 1977 msukumo mkubwa anaojivunia ni kuungwa mkono na vijana hasa wanawake.

“Kabla ya kuchukua fomu nimeshauriana na wengi wakiwemo Marais wastaafu lakini msukumo nilioupata zaidi ni kutoka kwa vijana na hasa wanawake,” alisema Karume ambae ni mtoto wa pili wa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume.

Balozi Karume ambae ana Shahada ya Uzamili (Master Degree) kutoka Chuo Kikuu cha Columbia nchini Marekani, aliwahi kusoma pamoja chuoni hapo na Rais wa sasa wa Marekani, Barack Obama wakati huo akichukua shahada ya kwanza aliyopita baada ya kutunukiwa Schorlaship na Rais wa kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere mwaka 1978, ingawa Obama alikuwa nyuma yake kwa mwaka mmoja.

Amesema akipata ridhaa ya wananchi ataongeza kasi kuimarisha uchumi na pato la mwananchi wa kawaida hasa kwa vijana.

Kila Mzanzibari aliyetimiza umri wa miaka kumi na nane anaweza kuandikishwa kuwa mpiga kura

Wataalamu wengi wa masuala ya siasa na sheria wanapendekeza taratibu mbali mbali za kuendesha uchaguzi wa viongozi.

Moja kati ya taratibu hizo ni kuwashirikisha wananchi wote katika kuchagua aina ya viongozi wanaowataka.

Katika kuwashirikisha huko wananchi lazima wawe huru kuchagua kiongozi wanaemtaka.

Kwa upande wa Zanzibar uchaguzi unaendeshwa kupitia Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, Sheria ya Uchaguzi namba 11 ya mwaka 1984, Kanuni mbali mbali zilizotungwa na Tume ya Uchaguzi pamoja na maelekezo mbali mbali ambayo hutolewa na Tume.

Katiba ndiyo iliyounda Tume ya Uchaguzi ambayo imepewa mamlaka ya kuendesha na kusimamia mchakato wote wa uchaguzi huku sheria ya Uchaguzi kwa upande wake ikiweka misingi na taratibu nyengine za uchaguzi wa Zanzibar.

Kanuni nazo zimefafanua baadhi ya mambo ambayo hayakuelezwa wazi katika sheria.

Pamoja na hayo Tume kupitia sheria ya uchaguzi inao uwezo wa kutoa maelekezo na ufafanuzi wa jambo lolote ambalo linahitaji kutolewa ufafanunuzi linalohusiana na uchaguzi.

Neno uchaguzi kwa mujibu wa sheria ya Uchaguzi Na. 11 ya mwaka 1984 limetafsiriwa katika hatua tatu tofauti.

Hatua ya kwanza ni uchaguzi wa Rais ambapo maana yake ni uchaguzi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

Hatua ya pili ni uchaguzi wa Baraza la Wawakilishi ambapo maana yake ni uchaguzi wa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na inajumuisha uchaguzi mdogo.

Hatua ya tatu ni uchaguzi wa serikali za Mitaa ambapo maana yake ni uchaguzi wa viongozi wa serikali za Mitaa ambao ni Madiwani na inajumuisha uchaguzi mdogo.

Tunaposema sheria ya uchaguzi inakusudiwa sheria Na. 11 ya mwaka 1984, sheria ambayo imeweka misingi na taratibu mbali mbali za uchaguzi kwa upande wa Zanzibar. Katika seria hii uchaguzi umegawika katika hatua kuu saba.

Kuandikisha wapiga kura, kufanya uteuzi wa wagombea, kufanya kampeni, kupiga kura, kuhesabu kura, kujumlisha kura na kutangaza matokeo.

Sheria hii ya uchaguzi imeweka utaratibu wa kila hatua tuliyoitaja hapo juu, hatua hizo zinawahusisha wananchi, vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi , kwa kuanzia hebu tujikumbushe hatua hizo walau kwa ufupi.

Kuandikisha wapiga kura

Katika zoezi hili, sheria imeweka wazi sifa za mtu kuweza kuandikishwa kuwa mpiga kura.

Kwa mfano kifungu cha 11 kinaeleza kuwa kila Mzanzibari aliyetimiza umri wa miaka kumi na nane (18) anaweza kuandikishwa kuwa mpiga kura kwa mujibu wa masharti ya sheria isipokuwa awe amezuiliwa kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi au sheria nyengine yoyote ile.

Hivyo, chini ya masharti ya sheria ya uchaguzi, ili mtu aweze kuandikishwa kama mpiga kura ni lazima awe na sifa zifuatazo.

Awe Mzanzibari; na awe na umri wa kuanzia miaka kumi na nane; na awe hajazuiliwa kuandikishwa na sheria.

Hizi ndizo sifa mama kwa mtu kuweza kuandikishwa kuwa mpiga kura kwa uchaguzi wa viongozi chini ya sheria ya uchaguzi.

Kufanya uteuzi wa wagombea

Kama tunavyojua kuwa uchaguzi unahusisha wagombea kutoka vyama tofauti vilivyopata usajili wa kudumu Tanzania.

Hivyo kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi jukumu la kufanya uteuzi wa wagombea ili waweze kushiriki katika uchaguzi lipo mikononi mwa Tume ya Uchaguzi.

Uteuzi wa wagombea nao umegawanyika katika hatua tatu tofauti kutegemea aina ya uchaguzi.

Uteuzi wa wagombea wa nafasi ya Urais; uteuzi wa wagomvea wa nafasi ya ujumbe wa Baraza la Wawakilishi; na uteuzi wa wagombea wa nafasi ya udiwani.

Uteuzi wa wagombea wa urais

Kifungu cha 31 kimeweka masharti ya uteuzi kwa wagombea wa kiti cha urais; masharti hayo ni kama yafuatayo.

Mgombea lazima awe anatoka kwenye chama cha siasa kilichosajiliwa.

Mgombea lazima awe amedhaminiwa na watu wasiopungua mia mbili waliondikishwa kuwa wapiga kura, kutoka katika kila mkoa katika mikoa mitano ya Zanzibar.

Taarifa za wagombea lazima ziwasilishwe kwa Tume katika fomu maalum itakayotolewa na Tume kwa kuwasilishwa katika afisi ya Tume ndani ya kipindi kilichowekwa na Tume; na

Mgombea kulipa fedha kama dhamana kiasi kama kitakachowekwa na Tume.

Mara baada ya hatua hizo kukamilika, Tume itafanya uteuzi kwa kuangalia sifa za mgombea kama zilivyoelezwa katika fomu iliyowasilishwa na baada ya kuridhika na sifa pamoja na masharti mengine, Tume itafanya uteuzi kwa kutangaza majina ya wagombea wa nafasi ya urais.

Uteuzi wa wagombea wa uwakilishi

Kwa upande wa nafasi ya ujumbe wa Baraza la Wawakilishi, sheria ya uchaguzi imeeleza utaratibu wa uteuzi katika kifungu cha 46, chini ya kifungu hichi yapo masharti makuu manne nayo ni:-

Mgombea lazima awe anatoka katika chama kilichosajiliwa;

Mgombea lazima awe amedhaminiwa na wapiga kura wa chama chake wasiopungua ishirini na tano ambao wameandikishwa kuwa wapiga kura katika eneo la uchaguzi lililomo ndani ya jimbo analotaka kugombea;

Taarifa za mgombea zitolewe katika fomu maalum iliyotolewa na Tume na kuwasilishwa kwa Tume ndani ya muda uliowekwa na Tume; na

Mgombea kulipa dhamana ya kima cha fedha kama kitakachowekwa na Tume.

Monday, June 21, 2010

Pindi tukizishinda changamoto hizi hakuna mtu atakaebakia pembezoni

Na Juma Khamis

KILA ifikapo May 9 ya kila mwaka, Umoja wa Ulaya (EU) huadhimisha siku yake kukumbuka siku ambayo Robert Schuman aliwasilisha pendekezo la kuundwa Muungano wa Ulaya mwaka 1950.

Pendekezo hilo lililopewa jina la "Azimio la Schuman", linachukuliwa kama mzizi uliosababisha kuuundwa kwa Umoja wa Ulaya.

Siku hii huadhimishwa kwa shughuli mbali mbali pamoja na matamasha yanayowakutanisha pamoja raia kutoka Muungano huo.

Siku hiyo pia huadhimishwa katika mataifa mbali mbali duniani, ambayo EU ina ushawishi wake ikiwemo Zanzibar.

Kwa mwaka 2010 Zanzibar ilikuwa mwenyeji, ambapo shughuli mbali mbali za maendeleo ya wananchi ambazo zinaungwa mkono na EU zilipewa kipaumbe cha kwanza.

Kwa mfano Balozi wa EU nchini Tanzania Tim Clarke, alipata fursa ya kukagua miradi ya kilimo katika maeneo mbali mbali ya Zanzibar, pamoja na kusikiliza changamoto zinazowakabili wakulima na wananchi kwa ujumla.

Clarke pia alipata fursa ya kusikiliza vilio kutoka kwa wananchi moja kwa moja au kupitia taasisi zinazowakilisha watu wanaoishi pembezoni, ambao idadi yao ni kubwa zaidi.

Licha ya jitihada kubwa zinazochukuliwa na EU, kuanzisha miradi mbali kwa lengo la kuwakomboa watu waliosahaulika, bado tatizo limebakia pale pale; matajiri wanaendelea kunawiri kwa utajiri na maskini wanaendelea kudidimia katika dimbwi la umaskini.

Tatizo ni kwamba miradi mingi inapoanzishwa na kuwa chini ya ufadhili, inawawia vigumu wananchi kuiendeleza baada ya mfadhili kuondoka.

Tatizo hili limejitokeza katika miradi kadhaa, ambayo sasa imekufa kabisa huku faida yake kwa wananchi ambao ndio walengwa ikiwa haionekani.

Tatizo jengine ni wananchi kutoshirikishwa kwa ukamilifu katika miradi husika huku wakipewa asilimia ndogo sana ya uendeshaji wa miradi.

Wao hawana nguvu ya kutumia fedha za miradi badala yake kutakiwa kuomba miradi kwa watu ambao walitakiwa tu kuwa wasimamizi na sio waendeshaji.

Changamoto zinazowakabili watu walioko pembezoni ni nyingi na zinaonekana katika mataifa mbali mbali duniani, lakini athari zaidi inajotokeza katika nchi maskini Zanzibar ikiwa miongoni mwao.

Makundi yaliyo pembezoni bado hayajaonekana ipasavyo na hayafikiwi na rasilimali muhimu za taifa (national cake) au zinawafikia kwa asilimia ndogo ambazo hazikidhi mahitaji yao wala hazitoshelezi kutoka na wingi wao.

Kwa mfano, vijana ambao ndio watu muhimu katika jamii bado wanakabiliwa matatizo makubwa ikiwemo upungufu wa ajira, ambapo zaidi ya asilimia 70 ya vijana hawana ajira za uhakika za kujipatia kipato.

Hali hii huwafanya wengi wao kujitumbukiza katika makundi maovu ya kutumia dawa za kulevya, wizi wa kutumia nguvu na ubakaji.

Ni kweli wizi haukubaliki katika jamii lakini kama kijana huyu angeandaliwa mazingira bora, bila shaka asingekuwa na muda wa kufanya uhalifu.

Lakini pia lazima ifike muda tukubali kuwa mfumo wetu wa elimu, haumsaidii kijana kujitegemea baada ya kumaliza shule.

Wapo wengi ambao wamemaliza elimu ya juu (shahada), lakini hawana kazi za kufanya na badala yake wanaendelea kuwa tegemezi kwa wengine.

Unyanyasaji mkubwa pia unaonekana kushamiri kwa wafanyakazi wa nyumbani, ambao daima wamekuwa wakilalamika lakini maskini sauti zao hazisikilikani na kama vile wameshindwa na mtu wa kuwatetea.

Hawa ni waathirika wa kulipwa mishahara midogo tena isiyo zingatia wakati, kiwango kidogo cha elimu, pamoja na udhalilishaji wa kimapenzi unaofanywa na waajiri.

Baba mwenye nyumba haoni tabu kumuomba penzi mfanyakazi wake wa ndani na kutishia kumfukuza pale anapokataa ‘kumuhudumia’.

Tatizo hili linaweza kuondoka tu kwa kuandaa mikataba kwa wafanyakazi wa ndani, kwa sababu kama zilivyo sekta nyegine sekta hii nayo ni muhimu.

Kundi jengine lililosahaulika ni la watu wenye ulemavu; kundi hili bado halifaidiki na mfumo wa elimu ulipo sasa, unyanyasaji unaofanywa na madereva, lakini pia mfumo wa miundombinu unaonekana haukuwazingatia watu wenye ulemavu.

Kwa mfano barabara hazijatengwa kwa watu wenye ulemavu, hali ambayo huwafanya kugongwa na madereva wazembe.

Changamoto nyengine zinazowakabili watu waliosahaulika ni kukithiri kwa matukio ya ubakaji kwa watoto wadogo, utelekezaji wa familia, upungufu wa miradi kwa wajasiriamali na ukosefu wa sheria zinazozingatia wakati na mazingira halisi yaliyopo sasa.

Kama kweli tutazimaliza changamoto hizi ni dhahiri hakuna mtu atakaebakia pambezoni.

Mwinyihaji aitaka Zantel iwasaidieni wananchi vijijini kunufaika na huduma za kibenki

Na Juma Khamis

WAZIRI wa Nchi (AR) anaeshughulikia fedha na uchumi, Dk. Mwinyihaji Makame, ametoa wito kwa kampuni ya simu za mkononi ya Zantel kuimarisha zaidi huduma zake hasa kwa watu wa vijijini Unguja na Pemba, ambao licha ya kuwa na simu za mkononi lakini wamekuwa wakishindwa kunufaika na huduma za kibenki.

Dk. Mwinyihaji aliyasema hayo jana wakati wa uzinduzi mpya wa huduma za Z- PESA inayotolewa na Zantel.

Alisema watu wa vijijini bado hawajanufaika vya kutosha na huduma za kibenki na kusema muda umefika sasa kwa Zantel kuwafikia kwa upana na haraka zaidi ili na wao waweze kufaidika na huduma hizo.

Kwa mfano alisema utumaji na upokeaji fedha kwa mfumo wa Z-PESA utawasaidia watu wa vijijini kupokea fedha kutoka kwa jamaa zao walioko nje ya Zanzibar kwa wepesi badala ya kwenda kupanga foleni benki ambazo zote zipo mijini.

Aidha alisema kwa kufanya hivyo, lile lengo la serikali la kupunguza umaskini kwa wananchi litaweza kufikiwa.

Waziri Mwinyihaji aliipongeza Zantel kwa kuendelea kuchangia huduma za maendeleo nchini na kuwa walipa kodi wa mwanzo nchini.

Nae Afisa Mtendaji Mkuu wa Zantel Noel Herrity, alisema Zantel kupitia mfumo wa Z- PESA imekusudia kubadili kabisa maisha ya Wazanzibari.

Herrity alisisitiza umuhimu wa kuleta karibu huduma za kibenki kwa wananchi walio wengi ambao hawapati huduma za kibenki ingawana wana simu za mkononi.

“Zantel tunafahamika kama kampuni bunifu ambayo inajitahidi kuwawezesha Watanzania kupata huduma za mawasiliano zilizo nafuu na katika mfumo huu wa Z PESA tutawaletea wateja wetu huduma za kibenki hasa wale ambao hawana fursa za kupata huduma hizo,” alisema Herrity.

Huduma hiyo za Z PESA imeongezewa huduma mpya ambazo zitawawezesha wateja wa Zantel Zanzibar kulipia na kununua bidhaa tofauti kama umeme maji, tiketi za ndege , kulipia DSTV (cable) pamoja na kutuma na kupokea fedha.

Afisa Mkuu wa Biashara wa Zantel, Norman Moyo alisema katika kufanikisha mfumo huo, Zantel imewahusisha wafanyabiashara, vyama pamoja na makundi yenye wanachama waliosambaa sehemu mbali mbali nchini kuwa mawakala wa Z -PESA.

“Zantel inawawezesha wafanyabiashara ndogondogo kukuza biashara zao katika maeneo mbali mbali ambayo hayajafikiwa na huduma za benki pamoja na kuwaongezea kipato,” alisema Moyo.

Huduma hizo mpya sasa itawawezesha Wazanzibari wenye ndugu zao ndani na nje ya nchi kupokea fedha kwa haraka zaidi.

Hata huvyo, watu waliohudhuria uzinduzi wa mfumo huo, wamesema elimu juu ya matumizi ya mfumo huo inapaswa kutolewa hasa kwa watu wa vijijini, vyengine mfumo unaweza kukosa uungwaji mkono.

“Bado mfumo ni mgumu na kama kweli Zantel wamedhamiria kuwasaidia kibenki hasa kwa watu wa vijijini wanapaswa kupita kila sehemu kutoa elimu kwa wateja wao,” walisema.

Serikali ya Mapindunzi ya Zanzibar inamiliki asilimia 18 ya hisa katika kampuni hiyo.

Balozi Karume: Kura yangu ya ndio au hapana itategemea nani atateuliwa kugombea Urais CCM

Na Juma Khamis
BALOZI wa Tanzania nchini Italia, Ali Abeid Amani Karume (60), amesema kura yake ya NDIO au HAPANA katika kura ya maoni kuamua mfumo wa uendeshaji serikali, itategemea nani atapitishwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) Julai 9 kuwa mgombea Urais wa Zanzibar katika uchaguzi mkuu ujao.

Kura ya maoni kuhusu mfumo wa serikali itafanyika Julai 31, takribani siku 20 baada ya CCM kuchagua mgombea wake wa Urais.

Balozi Karume aliyasema hayo hoteli ya Serena alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kuchukua fomu ya kuomba ridhaa kutoka chama chake kuteuliwa kuwa mgombea Urais wa Zanzibar.

“Tufikirie kwa makini kabisa kuunda serikali ya Umoja wa Kitaifa na mimi hili naliunga mkono lakini kura yangu ya NDIO au HAPANA itategemea mgombea wa Urais wa CCM atatoka upande upi,” alisema Karume.

Hata hivyo, alisema ni matarajio yake kwamba CC itawatendea haki wagombea wote na kuchagua mwanachama ‘asilia’ wa Zanzibar kugombea nafasi ya Urais wa Zanzibar.

“Tutashinda tukichagua kiongozi bora na si bora kiongozi,” alisema Balozi Karume huku akisisitiza kuwa kama atapitishwa na kushinda basi wala rushwa wataendelea tu kubakia na utaifa wa Zanzibar lakini wajiandae kutafuta nchi yao ya kuishi, akimaanisha kwamba atakabiliana kwa nguvu zake zote na mafisadi.

Akizungumzia nia yake ya kugombea kuteuliwa katika nafasi ya Urais, Balozi Karume ambae ni mdogo wa Rais wa sasa wa Zanzibar Amani Abeid Karume alisema: “Nimechangia vya kutosha Tanzania na sasa muda umefika kucha kuchangia nchini kwangu. Nia ninayo, sababu ninayo na uwezo ninao, nakiomba chama kinipitishe.”

Balozi Karume ambae ana kadi ya CCM No. AA 270259 aliyoipata Februari 5, 1977 msukumo mkubwa anaojivunia ni kuungwa mkono na vijana hasa wanawake.

“Kabla ya kuchukua fomu nimeshauriana na wengi wakiwemo Marais wastaafu lakini msukumo nilioupata zaidi ni kutoka kwa vijana na hasa wanawake,” alisema Karume ambae ni mtoto wa pili wa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume.

Balozi Karume ambae ana Shahada ya Uzamili (Master Degree) kutoka Chuo Kikuu cha Columbia nchini Marekani, aliwahi kusoma pamoja chuoni hapo na Rais wa sasa wa Marekani, Barack Obama wakati huo akichukua shahada ya kwanza aliyopita baada ya kutunukiwa Schorlaship na Rais wa kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere mwaka 1978.

Obama alikuwa nyuma yake kwa mwaka mmoja.

Wakati akichukua fomu, Balozi Karume ambae alikuwa karibu na Mabaunsa na mkewe ambao hata hivyo chanzo kimoja cha habari kilisema ni watoto wake, alisema atahakikisha anapata wadhamini kutoka mikoa yote mitano ya Zanzibar, ingawa sheria kwa kumgombea Urais ni kuwa na wanachama 250 kutoka mikoa mitatu ya Zanzibar.

Thursday, May 20, 2010

MUM: Chem chem ya maadili ya kiislamu

Na Juma Khamis

CHUO Kikuu cha Kiislamu Morogoro (MUM) ni taasisi binafsi ya elimu ya juu Tanzania iliyoanzishwa na Mfuko wa Maendeleo ya Waislamu (MDF).

MUM kilianzishwa chini ya mkataba maalum Oktoba 23 mwaka 2004 na kupata usajili kutoka Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU).

Dira ya MUM ni kuwa taasisi ya elimu iliyo imara na kituo kinachotoa elimu, ambayo inakidhi mahitaji ya jamii ya Kitanzania na dunia kwa ujumla, kwa kuzingatia misingi,miongozo na maadili ya kiislamu.

MUM pia kinajikita kuchangia juhudi za taifa za kutoa elimu bora inayokidhi mahitaji ya watu na soko bila kukiuka misingi ya dini.

Taasisi hii ni taasisi muhimu ya elimu hasa kwa jamii ya kiislamu, ambayo kwa muda mrefu sio kwamba ilinyimwa elimu lakini haikuwa na taasisi ya moja kwa moja ambayo ingetoa elimu kwa jamii hiyo.

Hivyo kwa kwa MUM inaonekana ni faraja kubwa kwa jamii ya Kiislamu Tanzania, Afrika Mashariki na dunia kwa ujumla, kwani ndio taasisi ambayo inawakutanisha vijana wengi wa kiislamu wenye madhebu tofauti, lakini lengo ni kujifunza kwa maslahi ya jamii inayowazunguka.

Kwa kuwa MUMU ni taasisi binafsi, wanafunzi wanaodahiliwa katika chuo hichi wanatrajiwa kuwa wawe na uwezo wa kujigharamia mafunzo yao, iwe kutoka kwenye mifuko, serikali au taasisi zisizokuwa na kiserikali (NGOs) au mashirika.

Serikali kupitia Bodi ya Mfuko wa Elimu ya Juu Tanzania (HESLB) imekuwa ikiwapatia mikopo wanafunzi wanaosoma chuoni hapo kwa lengo la kuwafanya wanafunzi wasome kwa utulivu.

Kwa kawaida HESLB huwalipia wanafunzi wa vyuo vikuu asilimia 100 iwapo mwanafunzi atakuwa amekidhi masharti, lakini mkopo huo hupungua kwa kadiri mwanafunzi anaposhindwa kukidhi masharti yaliyowekwa na Bodi.

Hata hivyo, upungufu huo hubakia kwenye ada ya masomo tu (tuition fee) lakini pesa za kujimu (accommodation) hulipwa sawa kwa wanafunzi wote, wale waliofadhiliwa kwa asilimia 100 na chini ya hapo.

Kwa MUM inapotokea mwanafunzi kufadhiliwa chini ya asilimia 100, gharama iliyosalia humlazimu mwanafunzi kuilipa mwenyewe kwa utaratibu uliopangwa na chuo.

Ada ya masomo kwa MUM inatofautiana sana na vyuo vikuu vyengine na hili limefanywa kwa kuzingatia hali halisi za Watanzania.

Kwa mfano mwanafunzi wa Kitanzania amekuwa akilipa shilingi 1,200,000 kwa mwaka na raia wa kigeni amekuwa akilipa dola za Marekani 2,100 kwa mwaka.

Gharama nyegine ni za matumizi ya kawaida ya mwanafunzi ambayo ni shilingi 1,835,000 ambazo mara nyingi hutolewa na Bodi ya Mfuko wa Elimu ya Juu.

MUM kimekua kikichua wanafunzi kutoka na uwezo wa chuo; kwa mfano katika mwaka masomo 2005, MUM kilikuwa na wanafunzi 167 kati yao 159 walihitimu shahada ya kwanza katika fani za sanaa, Uhusiano wa umma na masomo ya kiislamu Novemba 2008.

Kutoka mwaka wa masomo 2009/2010 MUM, kilipanga kuongeza idadi ya kozi kutoka tatu hadi saba.

Kozi hizo mpya ni Shahada ya Lugha , Shahada ya Biashara, Shahada ya Sayansi ya Elimu na Shahada ya Sheria na Shariah.

Udahili umekuwa ukifanywa kwa kuzingatia ushindani wa hali ya juu.

Kwa waombaji waliomaliza kidato cha nne na kukaa kusoma shule ya msingi kwa miaka saba, miaka minne sekondari na miaka miwili sekondari ya juu (kidato cha tano na sita), masharti ya chini ya kujiunga na MUM ni kuwa na ama kufaulu kwa alama mbili ambazo zitakuwa na uwezo wa kubeba pointi zisizopungua 4.5 au Diploma inayotambuliwa na inayolingana na maombi ya mwanafunzi.

MUM pia inaweza kumsajili mwanafunzi aliemaliza cheti kwa daraja lisilopungua la pili kwa masharti ya kuidhinishwa na Baraza la Senate la chuo.

Kwa wanafunzi ambao mfumo wao wa elimu unafikia miaka minane kwa shule ya msingi na miaka minne na sekondari ni lazima asome mwaka mmoja katika chuo cha nyumbani anakotoka.

MUM kina vifaa vya kisasa vya kujifunzia; ikiwa ni pamoja na vyumba vya kusomea vya kisasa, ambapo kila chuma kina uwezo wa kubaba wanafunzi 75, maktaba pamoja na fursa kadhaa za kujifunza.

Pia MUM kina kompyuta cha kutosha ambazo zimeunganishwa na mtandano wa internet, studio za redio na tv kwa wanafunzi wa shahada ya mawasiliano ya umma.

Chuo pia kina kampasi yake ambayo ina uwezo wa kuhudumia wanafunzi 600.

Ingawa MUM bado hakijajiunga na mfumo wa sasa wa kudahili wanafunzi kupitia kompyuta uliobuniwa na TUC, bado wanafunzi watakuwa na fursa za kufaidika na mikopo inayotolewa na HESLB.

Uamuzi wa kutojiunga TCU hautaathiri mustakabli wa MUM na wanafunzi kamwe hawapaswi kuhofia hilo, kwani MUM ni mwanachama wa TCU.

Uamuzi wa kujiunga au kutojiunga na TCU bado unabakia kuwa wa chuo, muhimu tu udahili ufanywe kwa kuzingatia masharti na mahitaji ya TCU.

Chuo Kikuu Morogo chawatoa hofu wanafunzi kuhusu mikopo

Na Juma Khamis

CHUO Kikuu cha Kiislamu Morogoro (MUM), kimesema uamuzi wake wa kutojiunga na mfumo wa mpya wa kusajili wanafunzi kupitia Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), hauathiri nafasi za wanafunzi kupewa mkopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Tanzania, (HESLB).

Taarifa iliyotolewa na ofisi ya Makamu Mkuu wa chuo hicho (Taaluma), kwa vyombo vya habari na Zanzibar Leo kupata nakala yake, imesema Bodi ya mikopo itaendelea na utaratibu wake wa kawaida wa kuwapatia mikopo wanafunzi wote wanaostahiki ambao watajiunga na MUM.

Kwa hivyo, wanafunzi wanaohitaji msaada wa fedha kutoka HESLB wanatakiwa kuomba kupitia bodi hiyo sambamba na kuomba udahili ambao utatolewa moja kwa moja na chuo badala ya TCU.

Kwa mujibu wa utaratibu mpya wa TCU, udahili kwa wanafunzi wanaojiunga na vyuo vikuu kuanzia mwaka wa masomo 2010/2011 utatolewa na tume hiyo na , badala ya mfumo uliozoeleka wa kuomba moja kwa moja kupitia vyuo husika.

Hata hivyo, TCU ilisema Chuo kikuu cha kiislamu Morogoro, Chuo Kikuu Zanzibar (ZU) kilichopo Tunguu na Chuo Kikuu cha Elimu Kishiriki Chukwani havijajiunga na mfumo huo na hivyo wanafunzi wanatakiwa kutuma maombi yao moja kwa moja vyuo husika.

Lakini wanafunzi walipata hofu wakiamini kuwa uamuzi wa vyuo hivyo kutojiunga na TCU ungewafanya kukosa mkopo unaotolewa na bodi ya mikopo na baadhi yao kuamua kutojiunga navyo.

Chuo hicho kimesema mfumo wa TCU ni wa hiari na hauna athari kwa vyuo vinavyokataa kuutumia.

Chuo cha Kiislamu Morogoro kimeanzishwa kuwasaidia wanafunzi ambao wamekosa fursa ya kujiunga na vyuo vyengine.

Tuesday, May 4, 2010

Tutaendelea kumkumbuka marehemu mzee Abeid Karume kwa mema aliyotufanyia

LEO ni Aprili saba,siku hii kwa Wazanzibari na Watanzania kwa Jumla inabakia kuwa nakumbukumbu muhimu.

Siku hii ya leo sote tunamkumbuka marehemu Mzee Abeid Aman Karume aliyeuawa kikatili na wapinga maendeleo.

Kifo chake kiliacha majo nzi na masikitiko makubwa sito tu kwa ndugu na wanafamilia lakini taifa letu la Tanzania , Afrika Mashariki na Afrika yote kwa jumla

Hali hiyo ilitokana na ukweli kwamba Marehemu Mzee Karume alikuwa ni dira sahihi katika kuleta kwanza ukombozi wa kweli wa Zanzibar lakini pia na maendeleo kwa jumla.

Sote tunafahamu kwamba mchango kwetu ulikuwa ni chachu muhimu ya kupata uhuru na hatimaye kuweza kujitawala baada ya kumuondoa Mkoloni na himaya zake.

Kwa ujumla wapinga maendeleo waliochukua kwa kuidhulumu kwa makusudi roho ya kiongozi wetu huyo mpendwa imetuweka kwenye majonzi makubwa tokea siku ya kifo chake na hadi leo tunaendelea kukumbuka.

Tunasema kutokana na umuhimu wake sote wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa jumla tutaendelea kukumbuka na kuuthamini kwa hali na mali mchango wake kwenye taifa leu.

Tunaahidi kutimiza na kuendeleza yale yote mazuri aliyoyanza na kuyadhamiria ya kuleta maendeleo ya kweli kwetu sisi wananchi,.

Mzee Karume kwa makusudi kabisa alipinga ubaguzi wa aina zote na kujitahidi kuwaunganisha wazanzibari wote na watanzania kwa jumla jambo ambalo leo hii tunajivunia kuwa na muungano madhubuti na wa aina yeka duniani.

Tunawaambia wale maahani hawakufanikiwa kuzima fikra sahihi za kimaendeleo za mzee wetu huyo licha ya kumkatili roho yake pasi na sababu yoyote.

Tutaendelea kuhudhunika kwa kuwa ni kipinze chetu na roho yake ilidhulumiwa lakini tutaungana kuendeleza masuala yote ya maendeleo ikiwemo huduma bora kwa jamii kama vile za makaazi bora , elimu , maji umeme , Afya na nyengine zote.

Kwa jumla sisi tunaamini kwamba kumuenzi mzee wetu huyu kwetu sisi sio jambo la bahati mbaya ila ni la dhamira ya kweli kwa kuwa alithubutu kujitolea hata kupoteza roho yake kwa sababu yetu sisi wazanzibar.

Hatuna cha kumlipa mzee wetu huyo zaidi ya kumuombea Mwenyezimungu amlaze mahali pema peponi nasi tukiamini kwamba siku moja tutakwenda huko ingawa yeye alidhulumiwa na mahani.

Tunaahidi kuwendelea kujitolea nafsi zetu katika kuhakikisha kwamba maendeleo ya wananchi wetu yanaimarika hatua kwa hatu ikiwa ni kutimiza malengo ya mapinduzi aliyoyaasisi kiongozi wetu huyo mpendwa.

Tunaami kwamba kufanya hivyo ndio kuitikia wito na dhamira ya kweli ya kumuenzi kwa vitendo kipenzi chetu huyo ambaye sote tunaendelea kuona kwamba kama ingekuwepo tungeza kupiga hatua kubwa ya kimaendeleo kuliko ilivyo sasa.

Monday, May 3, 2010

Tusherehekee uhuru wa habari kwa kuwasaidia wananchi badala ya kuwa ngazi

Na Juma Khamis

WAANDISHI wa habari duniani kote, jana waliadhimisha siku ya uhuru wa habari, ambao huadhimishwa kila ifikapo Mei 3 ya kila mwaka.

Waandishi wa habari hutumia fursa hii kujikumbusha na kutathmini changamoto mbali mbali wanazokabiliana nazo katika utekelezaji wa kazi zao ngumu.

Lakini pia hupata fursa ya kujifunza njia mpya za kupata habari pamoja na kuandika habari zaidi za uchunguzi ambazo haziegemei upande wowote, tena zikiwa na vianzio vingi (multiple sources) na kuachana na habari za fulani kasema, ambazo kimsingi hazipo kwa kuwasaidia wananchi.

Siku hii inaadhimishwa wakati Shirika la Kutetea Haki za Waandishi wa Habari Wasio na Mipaka (RWB) lenye makao yake makuu mjini Paris , Ufaransa likiwataja wakandamizaji wakuu 40 wa uhuru wa vyombo vya habari duniani.

Licha ya kwamba Shirika hilo hutoa orodha mpya kila mwaka , lakini kila mara hupatikana wale wanaoendelea kuziendea kinyume haki za uhuru wa vyombo vya habari.

Katika ripoti ya mwaka huu, Shirika hilo limewahusisha wanasiasa, viongozi wa kidini na viongozi wa makundi ya wapiganaji, makundi ambayo yalikuwa nadra kuyakuta katika ripoti zilizopita.

Kimsingi kila mtu ana haki ya kutoa mawazo yake, haki hii inajumuisha kuwa huru, uhuru wa kusema pamoja na kupata habari na fikra kutoka katika vyanzo vyovyote bila ya kuwekewa mipaka.

Kwa mujibu wa shirika hilo, makundi hayo yaliyotajwa kuwa yanakiuka uhuru wa kupashana habari, yana nguvu, ni hatari , hutumia nguvu na hayaguswi na sheria.

Watu hawa wanaokandamiza uhuru wa vyombo vya habari wana nguvu za kukagua habari, kuwaweka kizuizini waandishi habari, kuwateka nyara, kuwatesa na katika hali mbaya kabisa hata kuwaua.

Kwa bahati mbaya sana katika ripoti ya mwaka huu, Marais saba na viongozi kadha wa serikali wako katika orodha hiyo , ikiwa ni pamoja na rais wa China Hu Jintao, rais wa Iran Mahmoud Ahmedinejad, rais Paul Kagame wa Rwanda, Raul Castro wa Cuba na Waziri Mkuu wa Russia, Vladimir Putin, Waziri ambae alitarajiwa kuwa mtetezi mkubwa wa waandishi wa habari .

Wengine wapya katika orodha hiyo ambayo hupitiwa upya kila mwaka ya wakandamizaji wa haki za uhuru wa habari ni pamoja na mkuu wa kundi la Taliban, Mullar Mohammed Omar.

Kiongozi huyo wa Taliban , ambaye ushawishi wake umesambaa hadi Pakistan pamoja na nchi nzima ya Afghanistan , anajiunga na orodha hiyo kwa sababu kile kinachoitwa vita vitakatifu ambavyo anaviongoza ambavyo pia hulenga vyombo vya habari.

Viongozi hao huwatisha waandishi habari kwa sababu tu hawataki kuandika kuhusu mawazo yao binafsi, au ushindi hata pale wanaposhindwa.

Bila shaka vitisho kwa waandishi habari vinaimarisha hali ya raia kujenga hofu na kuelemea upande mmoja hata kama hawauungi mkono.

Kwa Tanzania, uhuru wa habari kinadharia unaonekana kukua kidogo, hasa baada ya serikali kuruhusu watu binafsi kuwekeza katika sekta ya habari.

Vyombo mbali mbali binafsi vimeanzishwa huku wananchi wakipata fursa pana zaidi ya kuvitumia.

Hata hivyo, tatizo bado liko katika upatikanaji wa habari nyeti ambazo zinaigusa moja kwa moja jamii, na ambazo ndio zinazotakiwa na jamii hiyo.

Kwa mfano, bado waandishi wa habari wamekuwa wakikabiliwa na matatizo wanapofuatilia habari zenye uhusiano na masuala ya rushwa au ukandamizaji wa haki za binaadamu.

Watoa habari nao ni changamoto nyegine katika kufanikisha uhuru wa habari. Wao wamekuwa woga kutoa ushirikiano kwa waandishi wa habari kwa kuhofia kupoteza nafasi zao au heshima katika jamii.

Zipo taarifa nyingi zinazowahusisha waandishi wa habari kukabiliwa na vitisho vya kuuawa kwa kisingizio cha kuingilia maslahi ya watu fulani pale wanaporipoti habari za upande mmoja baada ya kuchoshwa na urasimu walio nao viongozi ambao walipaswa kulizungumzia suala hilo kwa upande wa pili.

Changamoto nyegine, ni ile iyowakuta waandishi wa habari wenyewe kwa wenyewe, au taasisi moja ya habari na nyengine, na zaidi hili limejitokeza hapa Zanzibar.

Taasisi zinazosimamia masuala ya habari, zimekuwa zikikumbwa na migogoro ya ndani, ambayo yamesababisha baadhi yao kufa au kuzimia kabisa na kushindwa kufikia lile lengo la kuanzishwa kwake.

Hali hii inasababisha waandishi wa habari Zanzibar kushindwa kuwa na chombo cha kutetea maslahi yao.

Hata hivyo, katika kipindi hichi cha kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, waandishi wa habari wanaweza kuonekana watu kwa kuwa wako watu waliojiandaa kuwatumia kama ngazi kufikia malengo yao.

Hapa waandishi wa habari watatumiwa kuripoti hata msaada wa shilingi 10,000 kwa sababu tu mtu fulani anataka jimbo fulani.

Hivyo basi, tunapoadhimisha uhuru wa habari tukumbuke wajibu wetu wa kuisadia jamii badala ya wachahe wanaotaka kututumia kama ngazi.

Saturday, April 24, 2010

Utaratibu wa uendeshaji kesi za jinai

Na Juma Khamis
KATIKA mada hii tunakusudia kuanisha utaratibu wa kisheria kuhusu uendeshaji wa mashauri ya jinai.

Kimsingi ni muhimu kuweka bayana mambo ambayo kwa kiasi kikubwa yanagusa mwenendo mzima wa uendeshaji wa kesi za jinai na haki za wahusika yaani walalamikaji, watuhumiwa wa makosa, washitakiwa na wale waliopatikana na hatia.Wadau katika usimamizi wa haki katika mwenendo wa jinai ni jamii nzima kwa ujumla.

Hata hivyo, jamii inawakilishwa na vyombo vilivyopewa mamlaka kisheria.

Vyombo hivyo ni Mamlaka ya Upelezi yaani Polisi, Mamlaka ya Uendeshaji wa Mashtaka ambayo ni ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka na Mamlaka ya kusikiliza za kutoa uamuzi wa mashtaka hayo yaani Mahakama.

Hebu kabla hatujasonga mbele zaidi tuangalie makosa ya jinai na mashauri ya madai.

Ili kupata ufahamu wa kutosha na kuweza kuzingatia zaidi mada hii, ni vyema tukatofautisha walau kwa mukhtasari makosa ya jinai na mashauri ya madai.

Jinai kama ilivyotafsiriwa na vitabu mbali mbali vya sheria ni kutenda au kutokutenda jambo kunakomfanya mtu aadhibiwe kisheri.

Kwa ufafanuzi zaidi makosa ya jinai ni yale ambayo jamii inayaona bayana kuwa ni makosa yanayoigusa na mwenye kuyatenda anastahili kupewa adhabu kisheria.

Makosa haya yameanishwa katika sheria ya adhabu na katika vitabu vyengine vinavyohusika na upewaji adhabu kutokana na makosa mengineyo.

Kimsingi katika makosa ya jinai Dola, Jamhuri au serikali ndiyo hulalamika, kwa hivyo uhusiano wakisheria katika jinai ni baina ya mshitakiwa na Mamlaka ya nchi.

Kwa upande mwengine mashauri ya madai yanahusisha watu binafsi kutokana na kudaiana haki zao zinazotokana na mahusiano yatokanayo na makubaliano au kuaminiana kisheria ambapo mtu mmoja hakutekeleza makubaliano hayo au hakulipa anachodaiwa.

Madai kwa mujibu wa sheria hayahusishi adhabu bali mdaiwa hutakiwa kulipa au kutekeleza wajibu kutokana na makubaliano yaliyofikiwa.


Lakini kwa faida ya wasomaji, katika mada hii tutazingatia zaidi makosa ya jinai na jinsi ya kuyaendesha.

Mahakama zote zimepewa uwezo wa kusikiliza kesi za jinai kwa mujibu wa sheria.

Uwezo wa mahakama na mahakimu umeelezwa na sheria ya Mahakimu wa Mahakama za mwanzo, wilaya na za mkoa.

Ukubwa au umaalum wa kesi huzingatiwa katika kuamua ni mahakama ipi kesi ifunguliwe.

Katika kutekeleza hayo sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai imeeleza uwezo wa kutoa adhabu kwa mahakama zote.
Mahakama kuu ina uwezo wa kutoa adhabu yoyote au kutoa amri yoyote zilizoruhusiwa na sheria.

Kifungu cha 7 cha sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kinaeleza uwezo huo.

Kwa mujibu wa kifungu cha 8 cha sheria hiyo, mahakama ya mkoa imepewa uwezo wa kutoa adhabu ya kifungo kisichozidi miaka saba, faini isiyozidi shilingi milioni nne, kutumikia jamii kwa muda usiozidi miezi 12.

Mahakama ya wilaya nayo imepewa nguvu katika kifungu cha 9 kutoa adhabu ya kifungo kisichozidi miaka mitanom, faini isiyozidi shillingi milioni mbili na kutumikia jamii kwa kipindi kisichozidi miezi sita.

Kifungu cha 10 kinaipa uwezo mahakama ya mwanzo kutoa adhabu ya kifungo kisichozidi miezi mitatu, faini isiyozidi shilingi 100,000 na kutumikia jamii kwa kipindi kisichozidi miezi miwili.

Adhabu hizo za kutumikia jamii zimewekwa kwa mujibu wa kanuni za kutumikia jamii kanuni zilizotungwa na Jaji Mkuu.

Hata hivyo, kwa mujibu wa sheria ya mwenendo wa jinai, Mahakama ya mkoa imepewa uwezo wa kutoa adhabu kubwa zaidi hata kufikia kifungo cha maisha cha maisha ikwa baadhi ya makosa kwa mfano makosa yaliyotajwa na vifungu vya 125, 132, 150, 151, 160, 161, 286, 287, 324, 342(3),(4) na 343 vya sheria ya adhabu No.6/2004.

Mahakama hizo pia zaweza kuwa na nguvu zaidi iwapo zitapewa nguvu hizo na sheria ya Mahakimu wa Mahkama.

Kuhusu uwezo wa kusikiliza kesi za watoto (Juveniles) mahakama iliyopewa uwezo huo kwa mujibu wa sheria ni mahakama ya mkoa.

Watoto wasiozidi umri wa miaka 16 ndio husikilizwa katika mahakama za watoto.

Ukamataji, Upekuzi na Haki zake
Miongoni mwa hatua za awali kuhusiana na usimamizi wa m wenendo wa Jinai ni ukamataji na upekuzi wa watuhumiwa.

Namna ya ukamataji imeelezwa katika kifungu cha 13 cha sheria ya Mwenendo wa Jinai kwamba Polisi au mtu mwengine anapomkamata mtu analazimika kumgusa mtu huyo anayetakiwa kukamatwa.

Kifungu kidogo cha (2) cha kifungu hicho kinamtaka mkamataji kutumia kila njia muhimu kufanikisha ukamataji huo.

Ukamataji umegawanyika katika makundi mawili.

Ukamataji bila ya kutumia hati ya kukamata umeelezwa katika kifungu cha 21 cha sheria ya Mwenendo wa Jinai ambapo Polisi wanaruhusiwa kukamata watuhumiwa au wahalifu waliotenda au wanaotenda makosa yanayoonekana au kujulikana wazi wazi.

Zaidi ya makosa hayo yaliyotajwa na kifungu cha 21, makosa mengine yote yanayosalia yanahitaji kwanza hati ya kukamata (Arrest warrant), ambayo hutolewa na mahakama pekee.

Katika kufanikisha ulamataji, mambo mengine hutokea kama vile upekuaji wa eneo alilokamatwa mtuhumiwa kwa mujibu wa kifungu cha 14, ruhusa ya kuvunja ili kukamata au kuvunja ili kutoka iwapo mkamataji amefungiwa ndani kama kinavyoeleza kifungu cha 15.

Sheria pia inawapa watu binafsi au raia wa kawaida uwezo wa kukamata, kama ilivyoanishwa katika kifungu cha 26 na 44 kwa mahakimu kulingana na makosa na aina ya makosa hayo na namna yalivyotendeka.

Upekuzi: Hatua hii inahusu upekuzi wa watu na upekuzi wa maeneo.

Mtu aliyekamatwa hupekuliwa na Polisi na mali/vitu vyake au vilivyokamatwa miongoni mwake huhifadhiwa kwa mujibu wa kifungu cha 17.

Lakini kama tulivyoona awali eneo ambalo mtu anayekamatwa amepatikana hupekuliwa pia.

Sheria pia inawapa polisi uwezo wa kusimamia na kupukua gari na vyombo mbali mbali vya usafiri na usafirishaji iwapo kuna hisia au tuhuma za kuwepo mali au mhalifu katika vyombo hivyo kama ilivyoolezwa katika kifungu cha 18.

Lakini kifungu cha 19 kimezingatia stara ya mwanamke kwa kutana upekuzi wake ufanywe na wanawake wenziwe.

Kwa ujumla ukamataji na upekuzi ni matukio yanayokwenda pamoja na kwa mujibu wa sheria zipo haki ya msingi ambazo lazima zitekelezwe katika hatua hizo.

Haki za mtuhumiwa/mshitakiwa
Haki hizi zinaanzia wakati wa kukamatwa. Kifungu cha 30 kinamtaka mkamataji kujitambulisha na amweleze mkamatwaji makosa yake.

Haki nyegine ni ile ya kutowekwa ndani zaidi ya saa 24 bila ya kufikishwa mahakamani kama ilivyoanishwa katika kifungu cha 24.

Kifungu cha 32 kimakataza Polisi kumuweka mtu kizuizini bila ya sababu za msingi.

Mtu aliyekamatwa huhojiwa kuhusiana na tuhuma dhidi yake, hata hivyo kifungu cha 33 kinaelezea kwamba muda huo wa kuhojiwa usizidi saa nne au ikibidi kuongezwa muda huo kwa mujibu wa kifungu cha 34 basi usizidi saa nane au maombi ya kuzidishwa muda yapelekwe kwa Hakimu.

Tuesday, April 13, 2010

Wanaoomba Vyuo Vikuu sasa kutuma maombi TCU

Na Juma Khamis
UTARATIBU wa kujiunga na Vyuo Vikuu vya elimu ya juu nchini umebadilika na utaanza kutumika mwaka huu wa masomo 2010/2011.

Kwa mujibu wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), waombaji watatakiwa kuomba udahili moja kwa moja kupitia TCU kwa kutumia mtandao wa intaneti na simu za mkononi.

Utaratibu huo mpya unafuta ule wa zamani ambapo wanafunzi walikuwa wakituma maombi moja kwa moja vyuo vikuu.

Hata hivyo, utaratibu huo hautatumika kwa Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU) kilichopo Tunguu, Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Zanzibar Chukwani na Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro kwa kuwa havijajiunga na mfumo huo.

Wanafunzi wanaoomba katika Vyuo hivyo, watalazimika kutumia mfumo wa zamani wa kutuma maombi yao moja kwa moja chuoni.

Utaratibu huo mpya unawahusu wale watakaoomba udahili kwa kutumia sifa za kidatu cha sita , walizozipata kuanzia mwaka 1988 hadi mwaka 2010 na wale wenye vyeti vya nchi nyegine.

TCU imesema maombi kwa wanafunzi waliomaliza kidatu cha sita mwaka 1988 hadi mwaka uliopita na wale wenye vyeti vya nje yameanza tokea Aprili 8 mwaka huu.

Aidha Tume hiyo imesema kwa wale waliomaliza kidatu cha sita mwaka huu wataanza kuomba udahili Aprili 30 au wakati wowote majibu yao ta mitihani itakapotangazwa.

Saturday, April 10, 2010

Ijumaa kuu:Siku Yesu aliyosulubiwa msalabani

Na Juma Khamis (kwa msaada wa maandiko)
Leo ni Siku ya Ijumaa Kuu, ambapo wakristo duniani kote wanaungana wenzao, kukumbuka mateso aliyoyapata Yesu Kristo, wakati aliposulubiwa msalabani huko Jerusalem, yapata miaka 2, 000 iliyopita

Kumbukumbu hii, inaadhimishwa kwa ibada ya Ijumaa Kuu iliyojaa historia ya mateso ya Yesu Kristu.

Tendo la Yesu kufa msalabani linaonesha jinsi Yesu Kristu alivyokubali kubeba makosa ya wakiristu ikiwa ni fidia ya maisha kwa Mungu.

Hata hivyo, kufa msalabani hakuna maana kuwa Yesu alikuwa na dhambi.

Maandiko ya kikiristu (biblia) yanabainisha kuwa Yesu alikubali kuzibeba dhambi za wafuasi wake katika mwili wake juu ya msalaba, ili wapate kufa wakiwa hawana dhambi na kuishi kwa ajili ya uadilifu.

Kwa kadiri ya mafundisho ya Kanisa Katoliki, dhambi ni matendo yoyote ya makusudi ambayo mtu anayotenda kwa kwenda kinyume na mapenzi ya Mungu, yaani kuvunja amri 10 za Mungu.

Ili dhambi iitwe dhambi ni lazima itendwe kwa makusudi, yaani na mtu mwenye akili timamu.

Ijumaa kuu inaadhimishwa wakati dunia leo ikiwa imegubikwa na matendo mengi ya dhambi, huku matendo mazuri ya kumtukuza Mungu yakipungua na matendo mabaya ya kishetani yakitawala nafsi za watu na kusababisha watu waishi katika ulimwengu wa kutupiana mpira.

Serikali kwa upande inalaumu madhehebu ya dini, vivyo hivyo madhehebu ya dini yanailaumu serikali kwamba imekuwa laini mno kuruhusu na kuachia kila kitu, hata yale yanayokiuka maadili ya jamii

Kwa upande mwingine wazazi wanalaumu kuwa watoto wa siku hizi hawana heshima, watoto nao wanalaumu wazazi kuwa wao wamelegea katika suala la malezi, yaani wazazi wamekuwa huria mno katika suala la malezi na hawaishi na kutenda kulingana na umri wao.

Mfano mdogo tu, baba wa miaka 60 leo anafikishwa mahakamani kwa kulawiti mtoto wa miaka 12.

Pia kuna kutupiana mpira kati ya masikini na matajiri, kwamba maskini wanalalamika kuwa matajiri ndio chanzo cha uozo wote katika jamii, watu maarufu kujihusisha dawa ya kulevya na athari zake zinawakumba watoto wa maskini.

Pia mvutano mwingine ni kati ya nchi maskini na tajiri, Afrika inazilaumu nchi za Magharibi kuwa zinaua maadili ya Kiafrika kwa kusambaza utamaduni wake mchafu.

Lakini cha kujiuliza, hakuna sera zinazopaswa kuwekwa na nchi kama hizo kuzuia uingiaji wa tamaduni hizo?.

Kwa mfano, angalia suala la ndoa za mashoga, kuna nchi za Kiafrika zimeruhusu kufungisha ndoa za mashoga.

Ndio tendo la ushoga lilikuwepo lakini halikuwa limewekewa sheria ya kuliruhusu mpaka kwenye nyumba za ibada lifanyiwe ibada na kurasimishwa rasmi kuwa huyu mwanamume ni mke wangu na mimi mwanamume mwenziwe ni mume wake.

Sikuu ya Ijumaa kuu inafuatiwa na Pasaka ambayo historia yake imeanza mbali.

Siku hii ndio aliyofufukua Yesu Kiristu baada ya kusulubiwa msalabani.

Kabla ya kuja kwa dini ya Kikiristu, watu walikuwa na dini mbali mbali lakini baada ya kuanza, watu walianza kupuuza utamaduni wa kuabudu miungu na taratibu za watu wa mataifa mbali mbali, walianza kusherehekea sikukuu ya Pasaka, kama ishara ya kukubali utamaduni mpya.

Utamaduni mpya ulihimiza watu waache kuabudu miungu na kumfuata Yesu Kristo kama mfalme na mwokozi wa watu wote duniani.

Jina la Pasaka limetokana na neno la Kiebrania lenye maana ya pasaka.

Jina hilo lina maana ya kupita juu, kukaa juu au mlinzi kama ilivyoandikwa katika Biblia.

Sherehe za Pasaka ya Kikristo ni chimbuko la sherehe ya Pasaka ya Kiyahudi.

Kwa Kiswahili majina ya sherehe za Kikristo na Kiyahudi, hazitofautiani kwa kuwa tukio la kusulubiwa na kufufuka kwa Yesu Kristo lilitokea wakati wa sikukuu ya Pasaka ya Kiyahudi mwaka wa 30 kabla ya Kristo.

Kwa mujibu wa historia ya dini ya Kikristo, wakristo wa kwanza walikuwa Wayahudi.

Awali Wayahudi hao walikuwa wakisherehekea sikukuu ya Kiyahudi pamoja na kumbukumbu ya kufufuka kwa Yesu Kristo.

Hata hivyo, Wayahudi waliojikita kwenye dini ya Kikristo, waliamua kutenganisha sherehe hizo na kufuata kalenda tofauti, kwa lengo la kuimarisha dini ya Kikristo.

Pasaka ya Kiyahudi ni miongoni mwa sikukuu muhimu na yenye mtazamo wa kipekee kwa Wayahudi, kwani inatumika kukumbuka jinsi Wanaisraeli walivyofanikiwa kuwa huru, baada ya

Pasaka ya Kikristo inashabihiana sana na Pasaka ya Kiyahudi kutokana na historia ya Pasaka hizo mbili.

Kwa mujibu wa maandiko Musa alitumwa na Mungu kuwaondoa Wanaisraeli katika hali ya utumwa katika nchi ya Misri kisha kuwaongoza kwenda nchi ya ahadi.

Hata hivyo, mfalme wa Misri mwenye cheo cha Farao alikaidi amri ya Mungu na kuendelea kuwashikilia Wanaisraeli.

Kama ilivyo kwa Wayahudi, Pasaka ya wakristo inahesabiwa kuwa sikukuu muhimu kabisa katika ukiristo.

Tarehe ya Pasaka inafuata mwandamo wa mwezi, hivyo sikukuu hiyo haina tarehe maalumu katika kalenda ya kawaida.

Lengo la siku hii ni kuhimiza umoja aliokuwa nao Yesu Kristu kwani maandiko yanasema kabla Yesu Kristo hajasulubiwa msalabani alifanya karamu na kula pamoja na wanafunzi wake ili kuhimiza umoja na ushirikiano baina yao.

Kanali Kima atangaza kugombea Ubunge Chwaka

KANALI mstaafu wa JWTZ, Said Ali Khamis, maarufu Said Kima, ametangaza azma yake ya kugombea nafasi ya Ubunge katika Jimbo la Chwaka, kupitia chama tawala cha CCM.

Akizungumza katika mahojiano maalum nyumbani kwake Chukwani, Kima ambae aligombea nafasi hiyo katika uchaguzi wa mwaka 2005, alisema lengo lake ni kushirikiana na watu wa Chwaka kuliletea maendeleo Jimbo hilo.

Kanali huyo alishindwa na Mbunge wa sasa wa Jimbo hilo, Yahya Kassim.

Kima ambae aliwahi kuwa rubani wa ndege ya Rais wa serikali ya awamu ya pili ya Zanzibar, alisema anataka yale mazuri aliyoyapata kuyafanyia kazi kwa maslahi ya watu wa Chwaka na wilaya nzima ya Kati.

“Sina uwezo wa kuleta maendeleo peke yangu, lakini kwa sababu nimejifunza mengi mazuri, nitashirikiana na watu wa Chwaka kuhakikisha tunapata maendeleo,” alisema.

Mgombea huyo ambae ni mwanachama hai wa CCM alielipia kadi yake hadi mwaka 2013, alisema kama atashinda, Chwaka itakuwa Jimbo la mfano kwa maendeleo katika wilaya ya Kati.

Akizungumzia suala la elimu, Kima alisema inasikitisha kuona wilaya nzima ya kati haina skuli ya sekondari ya juu na hivyo, atahakikisha anatumia ushawishi alionao pamoja na wabunge wengine wa wilaya hiyo, kuipatia wilaya ya Kati skuli ya aina hiyo.

“Chwaka tumebahatika kuwa na Chuo Kikuu, lakini wanafunzi wengi wanaoingia pale ni kutoka nje ya Chwaka na wilaya ya kati, inasikitisha sana kuona tumeshindwa hata kuanzisha skuli ya elimu ya juu katika wilaya yetu,” alisema.

“Lazima tukubali kuwa wilaya ya Kati tuko nyuma sana kielimu na sasa muda umefika wa kusema basi na inatosha kuwa watu wa mwisho,” alisema.

Kanali Kima ambae aliwahi kuwa Mwenyekiti wa kwanza wa Bodi ya Mfuko wa Barabara Zanzibar, alisema lengo lake jengine ni kuhakikisha barabara ya Ukongoroni inajengwa kwa kiwango cha lami katika kipindi kifupi.

“Suala la Ukongoroni linanisikitisha, kama Mungu atanijaalia nikashinda, basi barabara hii itajengwa katika kipindi kifupi sana,” aliongeza.

Kujitangaza kwa Kima kunachukuliwa kama changamoto kubwa kwa Mbunge wa sasa, ambae kuna dalili ya kuomba kurejea tena katika Jimbo hilo kwa awamu ya nne (miaka 20), ingawa bado hajathibitisha.

Ni jukumu la mwari kumtaja mtu aliempa ujauzito

Na Juma Khamis
SHERIA ya kuwalinda wari na watoto wa mzazi mmoja, ni moja ya sheria nyingi zilizotungwa na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

Sheria hii ilitungwa kutokana na kukithiri kwa matukio ya udhalilishaji wa wari na watoto wadogo, lengo likiwa ni kukomesha unyanyasi huo.

Hata hivyo, licha kuwepo sheria hii, lazima tukiri kwamba bado vitendo vya kuwadhalilisha wari vimekuwa vikiendelea, huku wari wangi wakipewa ujauzito na kuishia kuolewa.

Sheria hii inaelezea kwa kina makosa mbali mbali ya jinai ambayo hayakuelezwa na sheria ya makosa ya Jinai (Penal Act No.6 ya mwaka 2004).

Kabla ya kuzungumzia baadhi ya makosa ya jinai katika sheria hii, kwanza tuone maana ya ‘mwari’ kama mmoja ya mlengwa wa sheria hii.

Kwa mujibu wa kifungu cha pili cha sheria hii, mwari ni mwanamke asiepata kuolewa ambaye yuko baina ya umri wa miaka 18 na miaka 21 na asiyepata kuzaa mtoto.

Baadhi ya makosa yanayotambuliwa na sheria hii ni pamoja mwari atakaepatikana na ujauzito ambao ameupata kwa hiari yake.

Adhabu katika kosa hili iwapo atatiwa hatiani ni kutumikia jamii kwa kipindi cha kuanzia miezi mitatu tokea siku aliyojifungua.

Sheria hii pia imebainisha kuwa mtu yeyote atakaehusika na ujauzito wa mwari huyo atakuwa amefanya kosa na pindi atakapotiwa hatiani adhabu yake ni kutumikia Chuo cha Mafunzo kwa kipindi kisichopungua miaka mitatu na si zaidi ya miaka mitano .

Pamoja na adhabu hiyo atatakiwa atoe matunzo kwa mtoto atakaezaliwa na mwari huyo.

Sheria pia imesema kuwa ni jukumu la mwari yeyote atakaekuwa mjamzito kutaja jina la mtu aliempa ujauzito huo na pindi mwari huyo atakataa kutaja jila mtu huyo atakuwa ametenda kosa la jinai na endapo atatiwa hatiani adhabu yake ni kutumikia jamii kwa kipindi cha miezi mitatu.

Hata hivyo, itakuwa ni kingi kwa mwari huyo kama atathibitisha kuwa ujauzito huo ameupata kutokana na kubakwa na watu wengi au mazingira mengine ambayo hakuweza kumtambua mbakaji.

Iwapo mwari huyo kwa makusudi amemtaja mtu tofauti na aliyemsababishia ujauzito huo, na kama mahakama itaridhika amefanya hivyo kwa makusudi, atakuwa ametenda kosa la jinai na akipatikana na hatia atatumikia jamii kwa kipindi cha miezi sita.

Friday, April 9, 2010

Magonjwa sugu ya macho sasa yatibiwa Z’bar

Na Juma Khamis
MAGONJWA sugu ya macho Zanzibar kama presha ya macho (glaucoma) na mtoto wa jicho sasa yanatibiwa nchini kwa kutumia teknolojia ya kisasa, inayotumiwa katika nchi kadhaa zilizoendelea ikiwemo Marekani na Ulaya.

Akizungumza katika mahojiano maalum na gazeti hili, daktari bingwa wa upasuaji wa macho kutoka China anaefanya kazi hospitali kuu ya Mnazimmoja, Dkt. Ji Jiangdong, alisema Zanzibar ni moja kati ya nchi zinazotumia huduma bora na ya kisasa zaidi katika kutibu maradhi ya macho.

Alisema wagonjwa wa macho sasa wana fursa sawa na zile wanazopata wagonjwa wenzao kutoka Marekani na mataifa ya Ulaya na katika baadhi ya miji nchini China.

“Hakuna upasuaji tunaofanya, badala yake tunatumia mashine maalum ambayo inanyonya mtoto wa jicho kwa kasi kubwa,” alisema Dkt Jiangdong.

Alisema mashine inayotumiwa ni aina ya Phacoemulsification ambayo ni ya kisasa na inapatikana katika hospitali kubwa duniani hasa nchi zilizoendelea na matibabu hufanywa kwa msaada wa Ultra Sound.

Aidha alisema mgonjwa anaefanyiwa matibabu sasa hapaswi kudungwa tena sindano, badala yake hutumia dawa maalum ya usingizi.

Alisema Zanzibar inapaswa kujivunia uhusiano wake na China kwani vifaa vilivyoletwa na serikali ya China havipo katika baadhi hospitali kubwa za mijini nchini humo.

“Hii ni huduma ghali sana duniani lakini kwa sababu Zanzibar na China ni marafiki wa karibu sana, tumeleta huduma hii ili watu wa Zanzibar nao wafaidike,” alisema.

Aidha alisema operesheni za macho kwa watoto wadogo, ambazo kabla zilikuwa zikifanyika katika hospitali ya CBRT kwa gharama za serikali ya Zanzibar sasa zinafanywa katika hospitali ya Mnazi mmoja.

Dkt. Jiangdong alisema asilimia 6.7 ya watu weusi wako kwenye hatari ya kuugua presha ya macho ikilinganishwa na watu weupe ambao ni asilimia 1-2.

Alisema mara nyingi huwapata watu walio na umri wa miaka 30-40 na 35-50.

Mapema Daktari dhamana wa kitengo cha macho katika hospitali hiyo, Dkt. Slim Mohammed, alisema gharama za matibabu kama hayo ambazo katika hospitali za Tanzania Bara zinafanywa kwa zaidi ya shilingi 400,000, kwa Zanzibar mgonjwa hutakiwa kuchangia shilingi 15,000 tu.

Aidha alisema kile kilio cha wananchi kudai kuwa viongozi wamekuwa wakifuata matibabu nje ya nchi sasa kimekwisha kwa kuwa viongozi wa juu wamekuwa wakipatiwa matibabu katika kliniki hiyo.

“Hakuna sababu kwa viongozi kufuata huduma ya macho nje ya nchi kwa sababu kile wanachokifata sasa kinapatikana Zanzibar,” alisema.

Gazeti hili lilimshuhudia Waziri wa Nchi, Afisi ya Rais, Mawasiliano na Uchukuzi, Machano Othman Said akipatiwa huduma ya macho katika kliniki hiyo.

Akizungumzia suala la wataalamu wazalendo watakaotoa huduma hiyo baada ya jopo la madaktari wa China kuondoka, Dkt. Mohammed alisema serikali tayari inasomesha wataalamu wake nchini China.

“Wataalamu wanzalendo tayari wako China na hivi karibuni tunatarajiwa watarejea kuanza kutoa huduma ya macho,” alisema.

Hata hivyo, alisema serikali ina mkataba na China kwa karibu miaka 10 wa kuwapatia madaktari bingwa wa fani tofauti.

Alisema matibabu ya presha ya macho mara nyingi hufanywa kwa kutumia dawa, upasuaji na hatua zinachukuliwa kutibu maradhi hayo kwa kutumia leser ambayo kwa sasa inatumiwa Afrika Kusini pekee.

Dkt. Mohammed alisema presha ya macho ni ugonjwa wa pili baada ya mtoto wa jicho unao
sababisha upofu Zanzibar.

Hivyo, aliwataka wananchi kuwahi hospitali haraka mara wanapoona dalili za kuumwa na kichwa au kutoona vizuri.

Tayari zaidi ya wagonjwa 600 wameshapatiwa matibabu ya macho tokea kuja kwa madaktari bingwa kutoka China, Unguja na Pemba na lengo ni kuwahudumia wagonjwa 1,400 kwa mwaka.

China ndio mfadhili mkuu wa kiliniki ya macho Zanzibar, ambapo imechangia vifaa vya kisasa vyenye thamani ya zaidi ya dola 800,000 pamoja na jopo la madaktari bingwa.

Uvimbe wa Ini sasa watibiwa bila kupasuliwa Mnazi Mmoja

Na Juma Khamis

KWA mara ya kwanza katika historia ya Zanzibar, madaktari bingwa wa upasuaji kutoka China, wamefanikiwa kuwafanyia upasuaji wagonjwa watano waliokuwa wakisumbuliwa na uvimbe wa usaha katika ini.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, daktari bingwa wa upasuaji Dk. Yong Shi, alisema wagonjwa hao walikuwa wakikabiliwa na ugonjwa unaosababishwa na mkusanyiko wa usaha katika ini (liver abscess).

Alisema upasuaji huo ambao ni wa kwanza kufanyika Zanzibar, umechukua dakika mbili tu kwa kila mgonjwa na unafanywa kwa utaalamu wa hali ya juu.

Upasuaji huo unaofanywa kwa muongozo wa Ultra Sound, ni wa kisasa na maarufu katika nchi nyingi duniani, lakini kwa Zanzibar ni mara ya kwanza kufanyika.

Mgonjwa hutobolewa sehemu ndogo ya tumbo na kupenyezwa kifaa maalum (tube) ambacho kwa wakati mmoja kina uwezo wa kutibu na kuingiza dawa kwenye sehemu iliyoathirika.

Dk. Yong alisema kabla ya teknolojia hiyo mpya kwa Zanzibar, mgonjwa kama huyo angelazimika kupasuliwa sehemu kubwa ya tumbo na kuondolewa sehemu iliyoathirika, kitendo ambacho ni hatari kwa maisha ya mgonjwa.

Alisema teknolojia hiyo, haina maumivu yoyote kwa mgonjwa na anaweza kupata nafuu katika kipindi kifupi tokea afanyiwe upasuaji.

“Upasuaji huu hauna maumivu kwa mgonjwa, mgonjwa anaweza kupona haraka, kuliko upasuaji uliokuwa ukifanywa kabla,” alisema Dk. Yong.

Alisema dalili za ugonjwa huo ni maumivu makali ya tumbo, homa na mgonjwa huwa hawezi kupinda.

“Kwa Zanzibar mgonjwa kama huyu angelazimika kufanyiwa upasuaji mkubwa na kukatwa sehemu kubwa sana ambayo inachukua muda mrefu kupona. Bila shaka upasuaji huu umefanikiwa kwa kiasi kikubwa, na tunajivunia,” alisema.

Akizungumzia ugonjwa wa vijiwe katika damu (blood stones), Dk. Shi alisema Wazanzibari wengi wanasumbuliwa na ugonjwa huo.

Aidha alisema, wengi wanaokwenda hospitali kwa kesi za kusumbiliwa uvimbe, vibofu vya mkojo au vijiwe kwenye damu ni wanaume na wanawake huenda hospitali wakiwa tayari wameshaathiriwa na maradhi hayo.

Mapema, mgonjwa Ali Juma ambae amefanyiwa upasuaji wa usaha katika ini aliliambia gazeti hili, kuwa maisha yake sasa yameokoka baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Juma ambae amehamishiwa hospitali ya Mnazi Mmoja akitokea hospitali ya Abdalla Mzee, Pemba, alisema kabla ya upasuaji alikuwa akipata maumivu makali ya tumbo na homa za mara kwa mara na kushindwa kufanya kazi zake vizuri kwa kuwa alishindwa kuinama na kupinda.

Akionekana mkakamavu, siku chache tu baada ya upasuaji huo, Juma alisema hali yake ya afya imerejea ya kawaida na hakuna maumivu yoyote aliyopata na anayopata baada ya upasuaji huo.

Dk. Shi alifanya upasuaji huo akisaidiwa na daktari wazalendo, akiwemo Dk. Suleiman Aboud Jumbe.

China yaipatia Zanzibar msaada

SERIKALI ya China imeipatia msaada wa vifaa mbali mbali vya kisasa vyenye thamani ya shilingi milioni 64 Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar vya uimarishaji wa huduma za afya katika Hospitali kuu ya Mnazimmoja.

Vifaa hivyo vitatumika katika hospitali ya Mnazimmoja kwa ajili ya huduma za upasuaji pamoja na sehemu ya macho.

Akipokea msaada huo Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Sultan Mohammed Mughery amesema kuwa China imefanikisha kwa kiasi kikubwa katika kuendeleza sekta ya afya kwa Unguja na Pemba.

Amesema msaada huo walioutoa utawezesha katika kufanya kazi hizo kwa urahisi na ufanisi mkubwa wa kuwahudumia wananchi wa Zanzibar.

Aidha Waziri Mughery amesifu jitihada za Serikali za China katika kuwapatia wataalamu mbali mbali ikiwemo wa maradhi ya wanawake kwa Hospitali kuu ya Mnazimmoja, macho pamoja na sehemu nyemgine.

Ameahidi kuwa vifaa hivyo vitatumika kwa uwangalifu ili viweze kudumu kwa muda mrefu na kusaidia utoaji wa huduma kuwa zenye ubora wa hali ya juu.

Nae kiongozi wa madaktari kutoka nchini China Dk Zhu Xiangjuan amesema nchi yake itaendeleza kila aina misaada kwa Zanzibar katika kustawisha maisha ya wazanzibari kwa huduma za afya.

Amesema wataendeleza kuwapatia madaktari vifaa pamoja na mafunzo kwa wafanyakazi wa Zanzibar ili waweze kuwahudumia wananchi kwa ufanisi wa hali ya juu.

China na Zanzibar imekuwa marafiki kwa kipindi cha miaka 46 sasa na wanaendelea kuisaidia Zanzibar katika nyanja tofauti ikiwemo madaktari pamoja na mambo mbali mbali na sasa wapo madaktari wapatao 21 ambao wanatoa huduma za kiafya kwa Unguja na Pemba.

Migomo katika maeneo ya kazi ni haki ya mwajiriwa

Na Juma Khamis
KATIKA safu hii leo alau kwa muhtasari tutaangalia asili ya uhusiano kati ya mwajiri na mwajiriwa mahapa pa kazi.

Kimsingi mwajiri tunaweza kumuelezea kama mtu (kampuni) mwenye kumiliki mtaji ambao unahitaji kutumika ili uwe na tija kwake, sio kama mwajiriwa.
Mwajiriwa ni yule mtu anaemiliki nguvu kazi ambao uhai na kustawi wake kunahitaji mtaji ili iweze kuwa na manufaa kwa muhusika.
Hapa ukiangalia utaona picha ya kutegemeana kati ya pande hizi mbili katika mikataba ya ajira (contract of service/ contract for service), yaani mtaji hautakuwa na manufaa yoyote kwa mwajiri endapo ataukalia nyumbani tu bila ya kuuwekeza.

Hivyo hivyo, mwajiriwa hatapata tija inayotokana na na nguvu kazi yake kama nguvu hizo ataamua kukaa nazo tu bila ya kuziwekeza kwe mwenye mtaji.

Kwa mantiki hiyo, kila upande unategemea upande mwengine.
Kutokana na hilo, ndipo tunapopata uhimuhimu wa mahusiano (relation) baina ya mwajiri na mwajiriwa katika mazingira ya kazi.
Lakini kama ilivyo kawaida, penye mkusanyiko mkubwa wa watu, migogoro na hali ya kutoelewana hasa kimaslahi sehemu ya kazi ni sehemu ya maisha na utamaduni uliozoeleka ingawa haupendwi sana na upande wa mwajiri.
Hii ni kwa sababu mwajiri siku zote anachotaka kuona kutoka kwenye mtaji wake ni faida tu na sio kitu chenginecho.
Ni kawaida katika maisha yetu kusikia migomo katika maeneo mbali mbali ya kazi na hata katika taasisi za elimu kama vyuo vikuu, ingawa kwa upande wetu Zanzibar matukio hayo ni machache kutokea, na pale inapotokea basi huwa kimya kimya na haileti athari kubwa.
Migomo mahala pa kazi ni kitendo cha wafanyakazi katika taasisi fulani kusitisha huduma zao.
Migomo hii imegawanyika katika sehemu mbali mbali kulingana na mbinu inayotumika kufanikisha mgomo husika.

Kwa mfano’ Go slow’ huu ni aina ya mgomo ambao kwa kawaida mwajiriwa hasitishi kutoa huduma zake, lakini anapunguza uzalishaji kiasi tu cha kumuathiri mwajiri.
Aina nyengine ya mgomo inaitwa ‘Pen down’ , katika aina hii ya mgono, mwajiriwa anafika kama kawaida yake katika sehemu yake ya kazi, lakini anasitisha kutoa huduma.
Aina hii inatofautiana na aina nyegine ya mgomo ambayo kwa jina la kisheria unaitwa ‘sit down’, katika aina hii mfanyakazi anafika sehemu yake ya kazi lakini anakataa kufanya kazi lakini pia anakataa kuondoka.
Mara nyingi, aina hii ya mgomo, hutumiwa vyombo vya usalama kuwaondoa wafanyakazi wanaokata kuondoka katika eneo la kazi.
‘Tool down’ hii ni aina ya mgomo, ambapo mfanyakazi anabakia katika sehemu yake ya kazi, lakini anasita kutoa huduma kwa kipindi kifupi, pengine dakika 10, saa moja na kadhalika.
Mgomo kama huu ulishawahi kufanywa na taasisi mbali mbali za fedha na athari yakae ikaonekana katka matawi ya taasisi hizo hapa Zanzibar.
Migomo mengine inayotambuliwa ni ‘lock out’ na ‘lock in’ ambapo mwajiriwa ama humfungia mwajiri wake nje ya ofisi (yaani humzuia kuingia ofisini) au humfungia mwajiri wake ndani ya ofisi (yaani kumzuia kutoka nje ya ofisi).
Kwa mwajiriwa mgomo ni ishara ya kuushinikiza uongozi (mwajiri) kutekeleza matakwa ya mfanyakazi.
Neno mgomo kama linavyosomeka, limebeba dhana nzima ya shari zaidi.

Kwa tafsiri ya mitaani, mgomo hutafsiriwa kama kitendo cha mwajiriwa kuasi na kukaribisha ghasia katika eneo la kazi, dhana ambayo haina mashiko ya kisheria.
Lakini katika hali ya mahusiano memea kazini, mgomo ni moja kati ya njia zinazokubalika kisheria kutumika kwa mfanyakazi kudai haki yake anayohisi kuwa imeporwa na ainaelekea kuporiwa na mwajiri.
Mgomo ni moja ya silaha inayokubalika kutumika kukabiliana na mwajiri ambae hataki kuthamini na kusikiliza kilio cha mtumishi wake.
Uhalali na uharamu wa mgomo utategemea malengo na jinsi utakavyotekelezwa.
Hapa naaminisha kuwa kuna maeneo mgomo haukubaliki.
Migomo kisheria huchukuliwa kama moja ya njia muhimu zinazowakutanisha ana kwa ana mwajiri na mwajiriwa na kutatua matatizo yao bila kuushirikisha upande wa tatu ambao unakua na udhaifu mkubwa katika kufikia maamuzi ya pamoja (collective agreement) kama ilivyoelezwa katika sheria ya mahusiano kazini No. 11 ya mwaka 2005.

Waandishi wa habari wanawajibika mbele ya sheria kwa makosa yanayotendwa na kalamu zao

SHERIA ya makosa ya jinai namba 6 ya mwaka 2004, imeeleza kwa kina baadhi ya makosa ambayo yanaweza kutendwa na waandishi wa habari.

Sheria hii imefafanua jinsi mwandishi wa habari anavyoweza kupatikana na hatia na makosa ambayo atayatenda na kuchukuliwa kama jinai dhidi ya Jamhuri.

Sheria hii imetambua kuwa mwandishi wa habari atakuwa amefanya kosa iwapo kwa kudhamiria au bila kudhamiria atachapisha habari za uongo ambazo zinaweza kusababisha fujo, hofu na kuchafua amani katika jamii.

Neno kuchapisha hapa halikutafsiriwa tu kwa vyombo vya habari vya kuchapisha (printing media) lakini hata kwa vyombo vyengine vya vya habari ambavyo kwa jina la kihabari vitambuliwa kama electronic media, mfano redio au televisheni.

Katika dunia ya sasa, vyombo vya habari vimekuwa vikutumika kwa njia moja au nyengine kuchapisha ama habari za uongo au habari zinazoegemea upande (single side story).

Kwa mfano katika mauaji ya halaiki ya Rwanda ya mwaka 1994, mahakama ya inayosikiliza kesi za mauaji hayo ICTR imewapata na hatia waandishi wa habari kadhaa kwa kutangaza habari za uongo au za uchochezi dhidi ya jamii moja.

Sheria hii ya mwaka 2006, pia imeeleza kuwa iwapo mwandishi wa habari atakutwa na hatia ya kuandika habari ya uongo na pindi atakapotiwa hatiani, adhabu yake haitazidi kifungo cha miaka miwili.

Hata hivyo, itakuwa ni kinga kwa kosa hili iwapo mshitakiwa atathibitisha kuwa kabla ya kuchapisha habari hiyo atakuwa amechukua hatua kuthibitisha usahihi wa habari hizo na kumpelekea kaumini kuwa habari hiyo ni ya kweli.

Kosa jengine ambalo sheria hii imelizingatia kwa mwandishi wa habari ni kuchapisha kitu chochote kwa lengo la kusomwa na kupelekea kushusha hadhi, kusababisha chuki au kashfa kwa mtoto wa Mfalme wa kigeni, Balozi, au kiongozi wa nje.

Au kwa lengo la kuchafua amani na urafiki kati ya Zanzibar na nchi ambayo mtu huyo anatoka.


Kosa jengine ni kuchapisha au kueneza jina au kitu chochote kitakachofichua jina la muathirika wa makosa ya kujamiiana (mfano mtu aliebakwa).

Adhabu kwa kosa hili ni kifungo kisichozidi miaka miwili au faini isiyozidi shilingi 300,000.

Isipokwa kama kuna amri ya maandishi ya afisa husika wa kituo cha polisi au afisa mpelelezi wa kosa hilo kwa nia njema (good faith) na kwa lengo la upelelezi, au kwa ruhusa ya maandishi ya muathirika (victim) au kama muathirika amefariki au ni mtoto mdogo au mwendawazimu kwa ruhusa ya jamaa wa karibu wa muathirika huyo na kwa ruhusa ya afisa husika wa kituo cha polisi.

Au kwa ruhusa ya mahakama katika kuchapisha jina la muathirika kinyume chake mtu atakaefanya hivyo bila ya ruhusa atakuwa amefanya kosa la jinai.

Ushahidi ni tegemeo muhimu kwa maamuzi ya mahakama

Na Juma Khamis
KIMSINGI mahakama ambayo ni moja ya mihimili mikuu mitatu ya dola, ndicho chombo chenye mamlaka ya kusikiliza au kuamua mashauri na kesi mbali mbali zinazoibuka miongoni mwa jamii.
Katika kusimamia na kutimiza wajibu wake kisheria hutegemea uwasilishaji wa ushahidi wa pande zote mbili katika kesi, yaani ushahidi wa upande wa mashtaka (Prosecution side) ambao kwa kawaida ndio unaoanzisha kesi na upande wa utetezi (Defensive side).
Ni kwa kuzingatia ushahidi huo ndio mahakama huwa na uwezo wa kupima na kuchambua kwa kina ushahidi uliowasilishwa kabla ya kuamua ni upande upi katika kesi una haki au upande upi umeshindwa kutokana na udhaifu wa ushahidi wake.
Kwa mujibu wa sheria ya ushahidi, ushahidi wa kusikia au kwa lugha ya kisheria ‘hear say evidence’ ni moja kati ya aina mbali mbali za ushahidi unaoweza kutumika katika kuthibitisha ukweli wa shauri lililofunguliwa mahakamani.
Hata hivyo, kimsingi aina hii ya ushahidi ni miongoni mwa ushahidi usiokubalika kutumika katika kuthibitisha kesi yoyote mahakamani, isipokuwa katika mazingira fulani.

Ushihidi wa kusikia, unatokana na maelezo ya kusikia kutoka kwa mtu mwengine ambaye ndiye aliyeshuhudia tukio lililoshuhudiwa.
Wanataaluma mbali mbali wa sheria (Jurists) wametafsiri kwamba ushahidi wa kusikia (Hear say Evidence) ni aina ya ushahidi ambao maelezo yake yametolewa na shahidi ambaye kimsingi hawezi kuutolea ushahidi mahakamani.
Yaani ushahidi ambao hutolewa na mtu ambae yeye binafsi hajashuhudia tukio, isipokuwa kwa kusikia tu kutoka kwa wengine.
Sababu ya kukataliwa kwa aina hii ya ushahidi katika kuthibitisha madai mahakamani ni kwamba haiwezekani katika hali ya kawaida kumuhoji shahidi juu ya kama hilo linalozungumzwa na mwengine ni la kweli au la.
Hii inawezekana pale tu inapotokea mtoaji halisi wa taarifa anapokuwa mahakamani kama shahidi, yaani shahidi aliyeshuhudia ukweli husika.
Sababu yengine inatokana na tabia ya kibinadamu. Hakuna mtu anaebisha kwamba ushahidi unaotolewa kwa kukariri au kurudia kilichosemwa na mwengine huwa na tabia ya kupotosha ukweli kwa kuwa kuna taarifa zitapunguzwa uhalisia wake na nyengine zitatiwa chumvi.
Sababu nyengine muhimu ni kutokana na wakati shahidi anapojaribu kurudia kauli ambayo aliitoa awali inakua na nguvu zaidi ikilinganishwa na kauli au taarifa za kusikia kutoka kwa mtu wa pili.
Kwa kawaida ushahidi hutengenezwa aidha kwa kuzungumza kwa mdomo au maelezo ya uthibitisho wa jambo, pia inaweza kwa kutumia mtindo wa kuwasilisha nyaraka (documents) zinazothibitisha ukweli mbele ya mahakama.
Pia inaweza kuhusisha aina yoyote ya mawasiliano ilimradi tu ni katika kuthibitisha.
Njia hizi zote zinaweza kuwa ni moja kwa moja au kupitia mtu mwengine.
Endapo ushahidi huo utatolewa kwa nia ya kutaka kuthibitisha uhalali kwa kauli iliyotumika, basi ushahidi huo utakuwa ni wa kusikia na hivyo hautakubalika mahakamani.
Ushahidi unaokubalika na mahakama ni ule wa kuthibitisha kauli inayothibitisha ukweli wa shauri au kesi hiyo.