Wednesday, July 28, 2010

Mgombea anaweza kutumia gharama zake mwenyewe wakati wa kampeni

Na Juma Khamis

KWA muda mrefu, Tanzania haikuwa na mfumo maalum wa kusimamia na kuratibu gharama za uchaguzi kwa gombea wa vyama vya siasa.

Katika uchaguzi wa mwaka 2010, kumekuwepo na mawazo na pia kujengeka utamaduni kwamba uongozi unaweza kununuliwa kwa fedha.

Tofauti za uwezo wa wagombea zimekuwa kubwa kiasi ambacho wananchi hawapati fursa ya kuchagua viongozi wanaowataka badala yake wale wenye fedha tu ndio wanachaguliwa kwa sababu ya fedha zao.

Baada ya kuona hali hiyo, serikali ya Tanzania iliona iko haja ya kuimarisha demokrasia ya uchaguzi kwa kuhakikisha kwamba kunakuwepo mazingira yaliyo salama na sawa kwa wagombea wakati wa uchaguzi ili kuweza kupata viongozi wenye uwezo wa kuongoza na kuwatumikia wananchi kwa ushawishi wa sera ya vyama vyao na sio fedha.

Katika kutimiza dhamira hiyo, serikali iliamua kutunga sheria ya gharama za uchaguzi namba 6 ya mwaka 2010 iliyopitishwa na Bunge Februari 11, 2010.

Hata hivyo, kwa kuwa sheria hii bado haijarasimishwa na Baraza la Wawakilishi kutumika katika mamlaka ya Zanzibar, haitakuwa na meno ya kuuma (haitafanya kazi) kwa nafasi za Urais wa Zanzibar, Uwakilishi na Udiwani, badala yake itatumika kwa nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Bunge (ingawa sheria ya uchaguzi kwa Wabunge wa Zanzibar inasimamiwa na sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar nambari 11 ya mwaka 1984).

Lengo la sheria hii ni kuutambua kisheria mchakato wa uteuzi wa wagombea ndani ya vyama vya siasa kuanzia ngazi ya kura za maoni na kusimamisha wagombea.

Kuweka utaratibu wa kisheria utakaosimamia na kuratibu mapato na kudhibiti matumizi pamoja na gharama za uchaguzi kwa vyama vya siasa na wagombea.

Kuweka viwango kwa matumizi na gharama za uchaguzi; kuweka utaratibu utakaosimamia mapato na matumizi ya vyama vya siasa ikiwa ni pamoja na zawadi, misaada na michango itakayotolewa na wagombea au wahisani wakati wa kampeni za uchaguzi.

Kudhibiti michango na zawadi kutoka nje, kuweka utaraibu na mfumo wa uwajibikaji wa mapato na matumizi ya fedha za uchaguzi kwa upande wa vyama vya siasa na wagombea na kuainisha adhabu kwa watakaokiuka masharti yaliyowekwa na sheria yenyewe.


Nini gharama za uchaguzi?

Gharama za uchaguzi maana yake ni fedha zote ambazo zimetumika au gharama zote zilizotumika kwa ajili ya kuendesha au kusimamia kura za maoni, kampeni za uchaguzi na uchaguzi kwa chama cha siasa, mgombea na serikali. Hii imeelezwa kwa kina katika kifungu cha 7(1) cha sheria ya gharama za uchaguzi.

Kwa hivyo, gharama ni matumizi yote yatakayohusika wakati wa kura za maoni ambayo yatakuwa yamegharamiwa na chama cha siasa, matumizi au gharama zozote zitakazo husika na chama ili kuwezesha uteuzi wa mgombea wake, gharama zozote au matumizi yoyote yatakayohusika na chama cha siasa au mgombea wakati wa kampeni ikiwa ni pamoja na gharama zote zitakazotumika kwa ajili ya vikundi vya uhamasishaji kwa ajili ya kumnadi mgombea.

Pia gharama za chakula, vinywaji, malazi au usafiri ambazo mgombea amegharamia wakati wa kampeni na gharama zozote au matumizi yoyote yatakayohusika na serikali, chama cha siasa au mgombea wakati wa uchaguzi yatajumuisha gharama za uchaguzi.

Sheria imeweka bayana kwamba kila chama cha siasa kitagharamia kampeni za uchaguzi kwa kutumia gharama za uchaguzi zinazotokana na vyanzo vyake, kwa mujibu wa kifungu cha 8(1) cha sheria hii.

Hata hivyo, kifungu cha 8(2) kimezingatia kuwa mgombea anaweza kutumia gharama zake mwenyewe wakati wa kampeni pale inapobidi kulingana na mahitaji ya kampeni zake.

Uwazi wa mapato na matumizi

Sheria hii inaweka sharti la uwazi katika mapato na matumizi ya vyama na wagombea kwa ajili ya uchaguzi kabla, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi.

Sheria hii pia inaelekeza utaratibu wa kufuatwa na vyama vya siasa na wagombea kutoa taarifa zao za mapato na matumizi ya uchaguzi, kama ilivyobainishwa katika kifungu cha 9(1) ambacho kinasema
“Mgombea atatakiwa kutoa taarifa ya fedha alizonazo na anazotarajia kupata na anakusudia kuzitumia kama gharama za uchaguzi ndani ya siku saba (7) baada ya siku ya uteuzi.”

Taarifa hizo zitawasiliskwa kwa Katibu Mkuu wa chama kwa mgombea wa nafasi ya Urais na kwa mgombea wa nafasi ya Ubunge taarifa zake ataziwasilisha kwa Katibu wa Chama wilaya.

Kila chama cha siasa kinachoshiriki katika uchaguzi ni lazima ndani ya siku thelathini (30) baada ya siku ya uteuzi wa wagombea kufanywa na Tume ya Uchaguzi kitoe taarifa kwa Msajili juu ya fedha zote ambazo kinakusudia kutumia kama gharama za uchaguzi; na kutumia kwa kuwadhamini wagombea wa chama hicho zikiwa ni kama gharama za uchaguzi.

Kanali Farrah atumia 99m/- kuimarisha chama, maendeleo ya jimbo Rahaleo

UPIGAJI kura ya maoni kwa wagombea Ubunge na Uwakilishi kwa tiketi ya CCM, itafanyika Agosti 1, siku moja tu baada ya Wazanzibari kupiga kura ya maoni kuhusu mfumo mpya wa serikali.

Kura hiyo inafanyika huku majimbo yakiwa yamefurika wagombea, hali ambayo haijawahi kutokea katika historia ya chama hicho.

Wagombea wa zamani wamekuwa wakijaribu bahati zao kwa mara nyengine tena huku wapya nao wakitaka kuingia kwa mara ya kwanza.

Miongoni mwao yumo Kanali mstaafu wa Jeshi, Saleh Ali Farrah, anaegombea tena nafasi ya Ubunge katika jimbo la Rahaleo.

Kanali Farrah anawania nafasi hiyo akiwa na matarajio makubwa ya kushinda, hasa kutoka na juhudi zake kubwa alizochukua katika kulijenga kimaendeleo jimbo la Rahaleo pamoja na chama cha Mapindunzi kwa ujumla.

Farah anasema, amefanya mengi ya kujivunia na ya kupigiwa mfano kwa wananchi wa Rahaleo, akisema maendeleo yaliyofikiwa hayajawahi kuonekana katika miaka kadhaa iliyopita.

Kanali Farrah anasema katika kipindi chake cha miaka mitano cha kuwatumikia wananchi wa Rahaleo, ametumia jumla ya shilingi milioni 99 kwa ajili ya kuleta maendeleo ya jamii, elimu, afya, michezo na kuimarisha shughuli za chama.

Farrah katika kipindi chake kilichomalizika pamoja na mambo mengine, ameweza kulipa posho kwa watendaji wa chama kila mwezi kati ya shilingi 10,000 na 30,000 kwa ngazi ya matawi, wadi na jimbo.

Malipo hayo ameyafanya katika kipindi cha miezi 56, ambayo yamemugharimu shilingi milioni 13,440,000.

Katika michango ya kuimarisha chama, Farrah kila mwezi amekuwa akitoa mchango wa shilingi 70,000 makao makuu ya CCM Kisiwandui, ambapo kwa Mkoa wa Mjini Magharibi amekuwa akichangia shilingi 40,000 wakati kwa wilaya ya mjini amekuwa akichangia shilingi 20,000 na kufanya jumla ya pesa alizochangia katika kipindi cha miezi 56 kufikia milioni 7,280,000.

Hakuishia hapo, kwa upande wa matembezi ya mshikamano, Kanali Farrah amechangia kila mwaka shilingi 200,000 na kufanya idadi ya fedha alizochangia katika matembezi hayo kufikia shilingi 1,000,000.

Katika uimarishaji wa maskani kaka ya Kisonge, Kanali Farrah amechangia shilingi 1,000,000 kwa maskani hiyo na kiasi kama hicho kwa maskani ya Kachorora ambazo ni maskani zenye nguvu kwa Zanzibar.

Akizungumzia uimarishaji wa wadi na jimbo, Farrah alisema amechangia mashine ya fotokopi kwa kila wadi ya jimbo hilo, huku Wadi ya Rahaleo ambao ina matawi matatu ikipatiwa shilingi 2,000,000 wakati Wadi ya Mlandege ambayo ina matawi manne akichangia shilingi 4,000,000.

Kanali Farrah, amekwenda mbali zaidi hata nje ya jimbo lake, anasema katika kufanikisha uchanguzi mdogo wa Magogoni, alichangia shilingi 1,000,000 wakati katika mfuko wa Mkoa wa kufanikisha uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 tayari ameshachangia shilingi 5,000,000 huku mfuko wa wilaya akichangia shilingi 1,500,000.

Katika matengenezo ya matawil ya Mwembeshauri, Rahaleo na tawi la Makadara, Kanali Farrah amechangia shilingi 9,750,000 huku katika daftari la kudumu la wapiga kura awamu ya kwanza, mwanajeshi huyo wa zamani alichangia shilingi 1,500,000 na awamu ya pili kiasi kama hicho cha fedha na kufanya idadi ya pesa alizochangia kufikia shilingi 3,000,000.

Ili jamii iweze kupata elimu bora, Kanali Farrah pia hakuwa nyuma akiamini kama kiongozi wa jimbo la Rahaleo huo ni wajibu wake.

Katika suala hilo, amechangia jumla ya shilingi 10,120,000 ikiwa ni pamoja mchango kwa wanafunzi wa michepuo wa skuli zilizomo ndani ya jimbo lake, tunzo kwa walimu, uchimbaji wa kisima kwa ajili ya wanafunzi na kumalizia ujenzi wa skuli ya msingi ya makadara.

Kwa kuwa Farrah pia ni mwanamichezo, muda wake mwingi amekuwa akiitumia kwa hali na mali kusaidia wanamichezo.

Tayari ametoa jezi seti moja yenye thamani ya shilingi 450,000 kwa klabu ya Mwembeshauri na klabu ya Rangers ya Makadara ambayo ilikabidhiwa seti ya jezi yenye thamani ya shilingi 250,000.

Aidha ametoa seti tatu za jezi kwa timu ya Jimbo na huduma nyengine kwa timu hiyo zenye thamani ya shilingi 4,500,000.

Mbali ya juhudi hizo alizochukua, pia amekuwa mstari wa mbele katika kukabiliana na tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama.

Katika nyanja hiyo, amechipa visima viwili katika Wadi ya Rahaleo kilichogharimu shilingi 3,000,000 na chengine Mwembeshauri ambacho kimegharimu shilingi 3,000,000.

Visima hivyo vyote vinatoa huduma kwa wananchi wa maeneo hayo kwa wakati wote.

Farrah pia amekiwa akiumwa na tatizo kwa watu wenye ulemavu; tayari amenunua viti vya walemavu kwa gharama ya shilingi 17,500,000 kuwasaidia wananchi ndani ya jimbo lake.

Katika kuvisaidia vikundi vilivyoanzishwa katika jimbo lake, Mbunge huyo anaemaliza muda wake ametumia wastani wa shilingi 1,500,000 kwa vikundi 15 kufungua vitabu vya benki ili kuweza kuendeleza shughuli zake.

Kwa watu wenye matatizo binafisi, Farrah ametumia shilingi 17,340,000 na anaamini bila ya msaada wao kumchagua katika uchaguzi wa mwaka 2005 asingeweza kutekeleza hayo.

Kanali Farrah anasema anarejea tena kuomba ridhaa ya wananchi jimboni akiwa msafi na akiamini kwamba amekamilisha yale ambayo wananchi walitaka ayatekeleze.

Farrah amewahakikishia wananchi wa Rahaleo kwamba, endapo watamchagulia tena watarajie maendeleo mapya ambayo yatakidhi mfumo wa sasa wa ilimwengu.

Farrah alizaliwa Juni 5, 1949 na kuanza elimu ya msingi katika skuli ya St Joseph Convent mwaka 1958 na kuhitimu mwaka 1965.

Baadae alijiunga na skuli ya Lumumba kuanzia mwaka 1966 hadi mwaka 1969 kabla ya kujiunga na chuo cha kijeshi mwaka 1980 hadi mwaka 1981.

Katika utumishi Farrah amelitumikia Jeshi la Wananchi wa Tanzania katika ngazi mbali mbali kuanzia mwaka 1971 hadi mwaka 1990 alipoteuliwa kuwa mlinzi wa Rais wa Zanzibar hadi mwaka 1999.

Katika kukitumikia chama alijiunga na ASP mwaka 1972, mbapo mwaka 1975 alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa tawi la ASP hadi mwaka 1976.

Mwaka 1977 alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa CCM hadi mwaka 1989.

Wednesday, July 21, 2010

Wagombea, mawakala wanayo haki ya kuhoji na kuangalia hatua za kujumlisha kura

Kuhesabu kura ni hatua inayofuata mara baada ya zoezi la kupiga kura kumalizika. Sheria ya uchaguzi imeweka utaratibu wa kuhesabu kura katika vituo vya kupigia kura.

Kwa kifupi, wasimamizi wa vituo vya kupigia kura ndio watakaohusika na kuhesabu kura vituoni.

Wakati wa kuhesabu vituo vya kupigia kura na maofisa wa kupiga kura, vitaitwa vituo vya kuhesabu kura na maofisa nao watakuwa maofisa wa kuhesabu kura.

Watu walioruhusiwa kuwemo katika vituo vya kupigia kura ndio watakaoruhusiwa kuwemo katika vituo vya kuhesabu kura.

Kifungu cha 80 cha sheria ya uchaguzi kimeweka utaratibu mzuri wa namna ya kuhesabu kura.

Lakini kabla ya kuhesabu kura msimamizi wa wa kituo atatakiwa kutoa taarifa zifuatazo kwa watu wanaoshikiri katika zoezi hilo.
Hesabu ya kura zilizopelekwa katika kituo cha kupigia kura
Hesabu za watu waliopiga kura
Hesabu ya kura zilizobakia ambazo hazikupigwa
Hesabu ya karatasi za kura
Idadi ya wapiga kura waliopiga kura, na
Hesabu za kura zote zilizotumika.

Na baada ya hapo, atakagua kifungio na kuhakikisha kuwa hakikufunguliwa au kufanyiwa udanganyifu, kufungua kifungio na kufungua sanduku tayari kwa kauanza kuhesabu kura.

Hatua hizi ni lazima zifuatwe ili kutekeleza yale matakwa ya kanuni na kisheria inayosema kwamba ‘sio tu kwamba haki itendeke bali ionekane bayana ikitendeka’.

Sheria inaelezea uwazi zaidi wa kuhesabu kura, kwa kumtaka msimamizi wa kuhesabu kura kukunjua karatasi ya kura na kutamka kwa sauti kilichoonekana katika karatasi hiyo, na hayo lazima yashuhudiwe na watu waliopo katika kituo cha kuhesabu kura.

Hata hivyo, ili kujua ipi halali na ipi batili, jukumu hilo limewekwa kwa Tume kwa kutunga kanuni kueleza ni ipi kura halali na ipi sio halali.

Hata hivyo, utaratibu unaotumika sasa ni kukubaliana kwa waliopo katika chumba cha kuhesabu kura, ipi kura halali na ipi kura batili.

Kujumlisha kura

Hii ni hatua inayofuata baada ya kuhesabu kura kutoka vituoni.

Ni hatua ambayo matokeo yote ya vituo vya kupigia kura hujumlishwa katika jimbo la uchaguzi ili kupata matokeo ya jumla kwa jimbo zima na hatimae kumpata mshindi.

Kifungu cha 83A kimewataja watu wanaoruhusiwa kuwepo wakati wa zoezi la kujumlisha matokeo ni.

(a) Msimamizi wa uchaguzi
(b) Msaidizi Msimamizi wa uchaguzi
(c) Mjumbe wa Tume
(d) Mkurugenzi wa Uchaguzi au Afisa wa uchaguzi wa Tume
(e) Mgombea
(f) Wakala wa kuhesabu kura
(g) Polisi au mtu mwenye jukumu la kuweka usalama katika kituo cha kuhesabu kura
(h) Waangalizi walioruhusiwa na Tume.

Wakati wa zoezi la kujumlisha matokeo, wagombea au wakala wao wanayo haki ya kuhoji na kuangalia hatua zote za kujumlisha kura na iwapo watakuwa na mashaka wanaweza kuomba kwa msimamizi wa uchaguzi ili kujiridhisha na ujumlishaji huo.

Aidha kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi, matokeo ya kura ya Urais yatajumlishwa na tofauti na yale ya Wawakilishi na Udiwani.

Kutangaza matokeo

Kutangaza matokeo ya uchaguzi ni hatua ya mwisho katika uchaguzi kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi.

Mamlaka ya kutangaza matokeo ya uchaguzi kwa ngazi zote yapo kwa Tume.

Kwa mujibu wa kifungu cha 88, inaelezwa kuwa, mara baada ya zoezi la kuhesabu na kujumlisha kura kukamilika na matokeo kuthibitishwa, Msimamizi wa uchaguzi atamtangaza mgombea aliyepata wingi wa kura halali.

Taarifa za matokeo pia zitapelekwa kwa maandishi kwa mshindi na baadae kutangazwa katika Gazeti rasmi la serikali.
Aidha kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi matokeo ya uchaguzi kwa uwakilishi na udiwani yatatangazwa na Wasimamizi wa uchaguzi wa Majimbo vituoni, na kwa ngazi ya Urais yatatangazwana Tume makao makuu.

Kwa maana hiyo, matokeo halali kwa mujibu wa sheria ni yale yatakayotangazwa na Tume na sio vyenginevyo.

Hizi ndizo taratibu za uchaguzi wa viongozi wa Zanzibar chini ya Sheria ya Uchaguzi Nam 11 ya mwaka 1984.

Thursday, July 15, 2010

Kampeni ya nyumba kwa nyumba ni kosa kwa mujibu wa sheria

Uteuzi wa wagombea wa udiwani

Ama kwa upande wa wagombea wa udiwani, masharti ya uteuzi yameelezwa katika kifungu cha 59 na 60, masharti yenyewe ni kama yafuatayo:

(a) Mgombea lazima awe amedhaminiwa na chama cha siasa kilichosajiliwa.

(b) Mgombea lazima awe amedhaminiwa kwa maandishi na wapiga kura wasiopungua kumi na tano (15) walioandikishwa kuwa wapiga kura katika eneo la uchaguzi analogombea.

(c) Mgombea alipe dhamana ya kima cha fedha kama kitakachowekwa na Tume.

Kama ilivyo kwa uteuzi wa wagombea wa urais, kwa upande wa uwakilishi na udiwani, baada ya hatua za chama au mgombea kuwasilisha fomu zao za kugombea kwa Tume, Tume itafanya uhakiki wa sifa na masharti mengine kama yalivyoelezwa na Katiba na Sheria ya uchaguzi, na baadae itafanya uteuzi wa wagombea waliotimiza sifa na vigenzo vilivyowekwa na katiba pamoja na sheria.

Kufanya kampeni
Kampeni ni hatua inayofuata baada ya uteuzi wa wagombea. Kwa kawaida kampeni hufanywa na chama au mgombea wa chama.

Hivyo sheria ya uchaguzi imeweka masharti ya kufuatwa na vyama au wagombea wakati wa kufanya kampeni kwa ajili ya uchaguzi.

Kifungu cha 56 kinaelezea kuwa kila chama kitawasilisha kwa Tume ya Uchaguzi ratiba ya mikutano ya kampeni inayoonesha wakati na pahali mikutano hiyo itakapofanyika na nakala ya ratiba hiyo kupelekwa kwa Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa wa Jeshi la Polisi kwa ajili ya kuandaa usalama wakati wa kampeni.

Tume inatakiwa kuhakikisha kuwa ratiba ya kampeni ya chama kimoja haigongani na ratiba ya chama chengine ili kuondoa hali ya kuwepo kwa kampeni mbili katika sehemu moja.

Sharti jengine lililowekwa katika kifungu hichi ni kwamba chama au mgombea kutofanya kampeni katika maeneo ya ibada au taasisi za taaluma.

Hata hivyo, maeneo ya taalamu au taasisi za ibada zimeelezwa kuwa ni maeneo yote yanayotumiwa na waumini kufanyia ibada ikiwemo misikiti, makanisa au madrasa au sehemu nyingine yoyote inayotumiwa na waumini kwa ajili ya ibada.

Aidha taasisi za taaluma ni sehemu yoyote inayotumika kwa ajili ya kutoa taaluma ikiwa ni pamoja na shule, vyuo na maeneo kwa hayo.

Pia sheria imepiga marufuku kufanya kampeni za nyumba kwa nyumba.

Kampeni za nyumba kwa nyumba ni kwa chama au mgombea kupita majumbani na kutangaza au kushawishi watu wapige kura chama au mgombea fulani.

Kupiga kura

Baada ya hatua ya kampeni kumalizika, hatua inayofuata ni kupiga kura. Sheria ya uchaguzi inasema kuwa Tume itatangaza siku ya kupiga kura na namna ya kupiga kura.

Zoezi la kupiga kura litafanyika katika vituo vya kupigia kura ambapo wapiga kura watatakiwa kufuata maelekezo yatakayotolewa na Tume juu ya utaratibu na namna ya kupiga kura, ikiwemo jinsi ya kujipanga kwa utaratibu maalum kama utakavyowekwa na kutangaza na Tume.

Hata hivyo, kupiga kura itakuwa kwa wale walioandikishwa na kupewa shahada za kupigia kura.

Kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi kila mtu atatakiwa apiga kura katika sehemu aliyoandilishwa kama mpiga kura katika eneo hilo, kinyume na hivyo mtu hatokuwa na haki ya kupiga kura.

Kuwepo utaratibu wa kuwawezesha wapiga kura wapige kura zao kwa njia ya siri na kwa upande wa wale watu wasioona, walemavu wa viungo au kushindwa kusoma, Tume ya uchaguzi inatakiwa kuanda utaratibu wa kuwawezesha watu wote hao wapige kura kwa namna iliyo huru, ikiwemo kuwaruhusu watu wao karibu kuweza kuwasaidia kupiga kura zao.

Vile vile sheria inaelekeza kuwa katika vituo vya kupigia kura, kutaruhusiwa watu maalum kuingia au kuwepo katika vituo hivyo. Watu watakaoruhusiwa kuwemo katika kituo cha kupigia kura ni:

(i) Mkuu wa kituo cha kupigia kura;
(ii) Msaidizi wa kituo cha kupigia kura
(iii) Wakala wa upigaji kura
(iv) Mpiga kura
(v) Mtu anayemsaidia mpiga kura mwenyewe ulemavu
(vi) Mwangalizi wa uchaguzi aliyepewa utambulisho na Tume
(vii) Mgombea
(viii) Mjumbe wa Tume
(ix) Mkurugenzi wa uchaguzi
(x) Afisa wa uchaguzi
(xi) Afisa wa polisi au mtu mwengine mwenye dhamana ya usalama katika kituo cha kupigia kura; na
(xii) Msimamizi wa uchaguzi na Msimamizi Msaidizi wa uchaguzi.

Hivyo kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi hawa ndio watu wanaoruhusiwa kuingia katika kituo cha kupigia kura.

Aidha mara baada ya zoezi la kupiga kura kumalizika, sheria inaelekeza utaratibu wa kuhidafhi masanduku ya kura baada ya kukubaliana na wahusika wote na kuyafunga namna ambavyo hayataweza kufunguliwa na hakuna chochote kinachoweza kuingizwa katika masanduku hayo.

Kuhesabu kura

Kuhesabu kura ni hatua inayofuata mara baada ya zoezi la kupiga kura kumalizika. Sheria ya uchaguzi imeweka utaratibu wa kuhesabu kura katika vituo vya kupigia kura.

Kwa kifupi, wasimamizi wa vituo vya kupigia kura ndio watakaohusika na kuhesabu kura vituoni.

Wakati wa kuhesabu vituo vya kupigia kura na maofisa wa kupiga kura, vitaitwa vituo vya kuhesabu kura na maofisa nao watakuwa maofisa wa kuhesabu kura.

Sunday, July 4, 2010

Dk. Shein: Msiwachague viongozi wachoyo, wabinafsi, wasiopenda umoja

WATANZANIA wametakiwa kuwa macho katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu na kuacha kuwachagua viongozi, wabinafsi, wachoyo na wanaopinga umoja nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Ali Mohammed Shein, alipozindua mbio za mwenge wa Uhuru mwaka huu kitaifa, uwanja wa Kwaraa, Mjini Babati Mkoani Manyara.

“ Msiwachague viongozi wachoyo, wenye ubinafsi kwa kuweka maslahi yao mbele, na hasa wale wenye kuwagawa wananchi na kudhoofisha umoja wa Taifa”Alisema Dk. Shein.

Aidha ametoa wito kwa vyama vya siasa na taasisi za kiraia, kushajiisha wananchi kujitokeza katika kupiga kura kwenye uchaguzi uliopangwa kufanyika nchini kote Oktoba mwaka huu.

“Uchaguzi huu utatoa fursa kwa wananchi kuchagua viongozi wenye uwezo wa kuleta maendeleo nchini na kudumisha umoja, amani na utulivu bila kuzingatia ukabila, rangi, dini, mitazamo yao kisiasa au jinsia zao” alifafanua Makamu wa Rais.

Akizungumzia rushwa katika uchaguzi mkuu, Dk. Shein alieleza kuwa lengo la kupambana na vitendo hivyo la Serikali ya awamu ya nne, linaendelea, ambapo amezitaka taasisi zote zinazohusika kwa njia moja au nyengine kwenye uchaguzi huo kuwajibika ipasavyo.

Pia Dk. Shein aliwasisitiza wananchi kuongeza nguvu ya kupambana na maradhi ya malaria, Ukimwi na dawa za kulevya, pamoja na kuacha na kulaani mauaji ya albino na kuwataja wahusika wa vitendo hivyo.

Aidha Dk. Shein, alieleza mkakati wa Serikali kuwapa kipaumbele watu walio katika makundi maalum, wakiwemo wenye ulemavu, wanawake, vijana na watoto kwa kuwawezesha, ili waweze kukabiliana na matatizo yanayowakabili.

Kwa mujibu wa waziri wa Kazi na Maendeleo ya Vijana, Prof. Juma Kapuya, mwenge wa uhuru mwaka huu utamaliza mbio zake Oktoba 14, Mkoani Kigoma.

Ujumbe wa Uhuru mwaka huu ni mapambano dhidi ya malaria, dawa za kulevya, Ukimwi na uchaguzi mkuu wa amani 2010.

Hata hivyo alisema pia mwenge huo mwaka huu utaendelea kukumbusha vita dhidi ya mauaji ya albino, rushwa na mambo yenye kuhusiana na haki za wanawake.

Sherehe hizo na uzinduzi pia zimehudhuriwa na Waziri wa Kazi, Maendeleo ya Vijana, Wanawake na Watoto Zanzibar, Asha Abdalla Juma, Waziri Mkuu Mstaafu, Fredrick Sumaye, Mkurugenzi wa ILO, wabunge na viongozi wengine wa vyama vya siasa na Serikali.
Mwenge huo mwaka huu utakimbizwa na vijana sita, wawili kutoka Zanzibar na wanne Tanzania Bara, ambapo kiongozi wao ni Nassor Ali Matuzya kutoka Mkoa wa Dar es Salaam.

Raza aota maisha bora kwa Mzanzibari

Juma Khamis
KADA wa CCM Mohammed Raza amesema maisha bora kwa Mzanzibari yanawezekana na ni jambo lisilo na mjadala.

Aidha alisema suala la Muungano halitahitaji tena kuzungumza na kamati, bali itakuwa ajenda kuu ambayo itazungumzwa na viongozi wa juu wa nchi na kusisitiza kwamba kasoro zilizopo sasa zitakuwa historia tu.

Alisema kulelewa kwake ikulu kumempa nafasi ya kufahamu mambo mengi na kwamba kama atateuliwa na kuwa Rais ataongoza kasi zaidi katika sekta ya elimu na uchumi.

Alikipongeza chama cha Mapindunzi kwa kuimarisha misingi ya demokrasia na utawala bora bila bila ubaguzi wa randi, dini au ukabila.

Balozi Karume asema hana tatizo na serikali ya Umoja wa Kitaifa

Na Juma Khamis

BALOZI wa Tanzania nchini Italia, Ali Abeid Karume (60), amesema kura yake ya NDIO au HAPANA katika kura ya maoni kuamua mfumo wa uendeshaji serikali, itategemea nani atapitishwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) Julai 9 kuwa mgombea Urais wa Zanzibar katika uchaguzi mkuu ujao.

Kura ya maoni kuhusu mfumo wa serikali itafanyika Julai 31, takribani siku 20 baada ya CCM kuchagua mgombea wake wa Urais.

Balozi Karume aliyasema hayo hoteli ya Serena alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kuchukua fomu ya kuomba ridhaa kutoka chama chake kuteuliwa kuwa mgombea Urais wa Zanzibar.

“Tufikirie kwa makini kabisa kuunda serikali ya Umoja wa Kitaifa na mimi hili naliunga mkono lakini kura yangu ya NDIO au HAPANA itategemea mgombea wa Urais wa CCM atatoka upande upi,” alisema Karume.

Hata hivyo, alisema ni matarajio yake kwamba CC itawatendea haki wagombea wote na kuchagua mwanachama ‘asilia’ wa Zanzibar kugombea nafasi ya Urais wa Zanzibar.

“Tutashinda tukichagua kiongozi bora na si bora kiongozi,” alisema Balozi Karume huku akisisitiza kuwa kama atapitishwa na kushinda basi wala rushwa wataendelea tu kubakia na utaifa wa Zanzibar lakini wajiandae kutafuta nchi yao ya kuishi, akimaanisha kwamba atakabiliana kwa nguvu zake zote na mafisadi.

Akizungumzia nia yake ya kugombea kuteuliwa katika nafasi ya Urais, Balozi Karume ambae ni mdogo wa Rais wa sasa wa Zanzibar Amani Abeid Karume alisema: “Nimechangia vya kutosha Tanzania na sasa muda umefika kuchangia nchini kwangu. Nia ninayo, sababu ninayo na uwezo ninao, nakiomba chama kinipitishe.”

Balozi Karume ambae ana kadi ya CCM No. AA 270259 aliyoipata Februari 5, 1977 msukumo mkubwa anaojivunia ni kuungwa mkono na vijana hasa wanawake.

“Kabla ya kuchukua fomu nimeshauriana na wengi wakiwemo Marais wastaafu lakini msukumo nilioupata zaidi ni kutoka kwa vijana na hasa wanawake,” alisema Karume ambae ni mtoto wa pili wa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume.

Balozi Karume ambae ana Shahada ya Uzamili (Master Degree) kutoka Chuo Kikuu cha Columbia nchini Marekani, aliwahi kusoma pamoja chuoni hapo na Rais wa sasa wa Marekani, Barack Obama wakati huo akichukua shahada ya kwanza aliyopita baada ya kutunukiwa Schorlaship na Rais wa kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere mwaka 1978, ingawa Obama alikuwa nyuma yake kwa mwaka mmoja.

Amesema akipata ridhaa ya wananchi ataongeza kasi kuimarisha uchumi na pato la mwananchi wa kawaida hasa kwa vijana.

Kila Mzanzibari aliyetimiza umri wa miaka kumi na nane anaweza kuandikishwa kuwa mpiga kura

Wataalamu wengi wa masuala ya siasa na sheria wanapendekeza taratibu mbali mbali za kuendesha uchaguzi wa viongozi.

Moja kati ya taratibu hizo ni kuwashirikisha wananchi wote katika kuchagua aina ya viongozi wanaowataka.

Katika kuwashirikisha huko wananchi lazima wawe huru kuchagua kiongozi wanaemtaka.

Kwa upande wa Zanzibar uchaguzi unaendeshwa kupitia Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, Sheria ya Uchaguzi namba 11 ya mwaka 1984, Kanuni mbali mbali zilizotungwa na Tume ya Uchaguzi pamoja na maelekezo mbali mbali ambayo hutolewa na Tume.

Katiba ndiyo iliyounda Tume ya Uchaguzi ambayo imepewa mamlaka ya kuendesha na kusimamia mchakato wote wa uchaguzi huku sheria ya Uchaguzi kwa upande wake ikiweka misingi na taratibu nyengine za uchaguzi wa Zanzibar.

Kanuni nazo zimefafanua baadhi ya mambo ambayo hayakuelezwa wazi katika sheria.

Pamoja na hayo Tume kupitia sheria ya uchaguzi inao uwezo wa kutoa maelekezo na ufafanuzi wa jambo lolote ambalo linahitaji kutolewa ufafanunuzi linalohusiana na uchaguzi.

Neno uchaguzi kwa mujibu wa sheria ya Uchaguzi Na. 11 ya mwaka 1984 limetafsiriwa katika hatua tatu tofauti.

Hatua ya kwanza ni uchaguzi wa Rais ambapo maana yake ni uchaguzi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

Hatua ya pili ni uchaguzi wa Baraza la Wawakilishi ambapo maana yake ni uchaguzi wa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na inajumuisha uchaguzi mdogo.

Hatua ya tatu ni uchaguzi wa serikali za Mitaa ambapo maana yake ni uchaguzi wa viongozi wa serikali za Mitaa ambao ni Madiwani na inajumuisha uchaguzi mdogo.

Tunaposema sheria ya uchaguzi inakusudiwa sheria Na. 11 ya mwaka 1984, sheria ambayo imeweka misingi na taratibu mbali mbali za uchaguzi kwa upande wa Zanzibar. Katika seria hii uchaguzi umegawika katika hatua kuu saba.

Kuandikisha wapiga kura, kufanya uteuzi wa wagombea, kufanya kampeni, kupiga kura, kuhesabu kura, kujumlisha kura na kutangaza matokeo.

Sheria hii ya uchaguzi imeweka utaratibu wa kila hatua tuliyoitaja hapo juu, hatua hizo zinawahusisha wananchi, vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi , kwa kuanzia hebu tujikumbushe hatua hizo walau kwa ufupi.

Kuandikisha wapiga kura

Katika zoezi hili, sheria imeweka wazi sifa za mtu kuweza kuandikishwa kuwa mpiga kura.

Kwa mfano kifungu cha 11 kinaeleza kuwa kila Mzanzibari aliyetimiza umri wa miaka kumi na nane (18) anaweza kuandikishwa kuwa mpiga kura kwa mujibu wa masharti ya sheria isipokuwa awe amezuiliwa kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi au sheria nyengine yoyote ile.

Hivyo, chini ya masharti ya sheria ya uchaguzi, ili mtu aweze kuandikishwa kama mpiga kura ni lazima awe na sifa zifuatazo.

Awe Mzanzibari; na awe na umri wa kuanzia miaka kumi na nane; na awe hajazuiliwa kuandikishwa na sheria.

Hizi ndizo sifa mama kwa mtu kuweza kuandikishwa kuwa mpiga kura kwa uchaguzi wa viongozi chini ya sheria ya uchaguzi.

Kufanya uteuzi wa wagombea

Kama tunavyojua kuwa uchaguzi unahusisha wagombea kutoka vyama tofauti vilivyopata usajili wa kudumu Tanzania.

Hivyo kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi jukumu la kufanya uteuzi wa wagombea ili waweze kushiriki katika uchaguzi lipo mikononi mwa Tume ya Uchaguzi.

Uteuzi wa wagombea nao umegawanyika katika hatua tatu tofauti kutegemea aina ya uchaguzi.

Uteuzi wa wagombea wa nafasi ya Urais; uteuzi wa wagomvea wa nafasi ya ujumbe wa Baraza la Wawakilishi; na uteuzi wa wagombea wa nafasi ya udiwani.

Uteuzi wa wagombea wa urais

Kifungu cha 31 kimeweka masharti ya uteuzi kwa wagombea wa kiti cha urais; masharti hayo ni kama yafuatayo.

Mgombea lazima awe anatoka kwenye chama cha siasa kilichosajiliwa.

Mgombea lazima awe amedhaminiwa na watu wasiopungua mia mbili waliondikishwa kuwa wapiga kura, kutoka katika kila mkoa katika mikoa mitano ya Zanzibar.

Taarifa za wagombea lazima ziwasilishwe kwa Tume katika fomu maalum itakayotolewa na Tume kwa kuwasilishwa katika afisi ya Tume ndani ya kipindi kilichowekwa na Tume; na

Mgombea kulipa fedha kama dhamana kiasi kama kitakachowekwa na Tume.

Mara baada ya hatua hizo kukamilika, Tume itafanya uteuzi kwa kuangalia sifa za mgombea kama zilivyoelezwa katika fomu iliyowasilishwa na baada ya kuridhika na sifa pamoja na masharti mengine, Tume itafanya uteuzi kwa kutangaza majina ya wagombea wa nafasi ya urais.

Uteuzi wa wagombea wa uwakilishi

Kwa upande wa nafasi ya ujumbe wa Baraza la Wawakilishi, sheria ya uchaguzi imeeleza utaratibu wa uteuzi katika kifungu cha 46, chini ya kifungu hichi yapo masharti makuu manne nayo ni:-

Mgombea lazima awe anatoka katika chama kilichosajiliwa;

Mgombea lazima awe amedhaminiwa na wapiga kura wa chama chake wasiopungua ishirini na tano ambao wameandikishwa kuwa wapiga kura katika eneo la uchaguzi lililomo ndani ya jimbo analotaka kugombea;

Taarifa za mgombea zitolewe katika fomu maalum iliyotolewa na Tume na kuwasilishwa kwa Tume ndani ya muda uliowekwa na Tume; na

Mgombea kulipa dhamana ya kima cha fedha kama kitakachowekwa na Tume.