Monday, January 31, 2011

Bado sekta ya utalii inahitaji kuangaliwa zaidi

ZANZIBAR kwa kiasi kikubwa inategemea mchango wa sekta ya utalii katika pato lake la taifa, sekta ambayo imeamza kuimarika nchini.

Sekta hiyo inatoa mchango mkubwa kwa sababu ni sekta inayoweza kukua na kutumika kuwavutia wageni kutoka nje kutokana na historia ya nchi na pia mnasaba wake kwa wageni kuwa sehemu ya vivutio vya wageni hao.

Ni jambo la kujivunia kuona kuwa tangu serikali ilipoanzisha sekta hiyo miaka kadha sasa, imeweza kuongeza pato linalotokana na utalii huku hoteli nazo zikiongezeka, hali inayowafanya wageni wengi kuja nchini.

Kama ilivyo kwa sekta nyengine za kuchangia uchumi sekta hiyo pia inakumbwa na matatizo ya hapa na pale kwa sababu inawahusisha binadamu hivyo haiwezi kukosa misuko suko ndani yake.

Hivi sasa kuna malalamiko mengi ndani ya sekta hiyo lakini mengi yanaweza kutatuliwa kwa sababu yanafanywa na binadamu.

Wapo wanaolalamika kukoseshwa ajira katika hoteli za kitalii na badala yake ajira nyingi zimeelekezwa kwa wageni ambao nao pia ni wengi kijumla katika ajira hizo huku wananchi na hasa wazalendo wanaotoka kwenye vijiji vya jirani wakishuhudia.

Matatizo mengine makubwa ambayo ni mazungumzo ya kila siku ni udhaifu unaofanywa na wawekezaji wa kuwadhulumu wafanyakazi mafao yao pamoja na kuwadhalilisha katika kazi hizo na hasa pale wanapodai mishahara yao ambayo hulipwa bila kuzingatia sheria zinazosimamia kazi hiyo.

Kwa kawaida migogoro ya namna hiyo hutakiwa ifanyiwe marekebisho haraka mara baada ya wahusik kufikisha malalamiko yao kwenye vyombo husika.

Pamoja na kuwepo miongozo na sheria za kuzingatiwa lakini wafanyakazi hao wamekuwa wakihangaishwa sana na waajiri na inapotokea kufikisha malalamiko yao katika ngazi ya juu basi hufukuzwa kazi ama kurudishwa kazini kwa kuajiriwa bila mikataba.

Kero hizo zimekuwa zikisikika kila mara lakini maamuzi yanayofikiwa huwa ya kubabaishwa kutokana na uhusiano uliopo kati ya viongozi na waajiri wa hoteli, hali inayonesha mara nyingi kuwepo kwa harufu ya rushwa ndani yake.

Baadhi ya maofisa wanmaopewa jukumu hilo hushirikiana na wageni “kuwanyonga” wenyeji wanapokwenda kudai haki hizo.

Jambo hilo limejitokeza kuwa sehemu ya vikwazo vinavyochangia kasoro zinazojitokeza mara kwa mara katika sekta ya utalii.

Hali hiyo mara kadha imekuwa chanzo cha wamiliki wa hoteli kuikoseha mapato serikali kwa kushirikiana na maofisa wazalendo katika taasisi za umma.

Ninadhani matukio ya udhalilishaji wa aina mbali mbali ni mengi katika sekta hiyo lakini hayafikii mbali kwa vile watetezi wa wafanyakazi hao wanaangalia zaidi maslahi yao badala ya muajiri wake na kutowahurumia ndugu zao wanopata madhila mbele ya wageni.

Hivyo,ni jukumu la serikali sasa kutafuta wawekezaji wenye uwezo wanaoweza pia kuwathamini wafanyakazi wao ambao ndio msingi wa mapato yao ya kila siku.

Hivi hali hii ya kunyanyaswa wafanyakazi wetu itaendelea hadi lini, kwani inalalamikiwa vya kutosha lakini wawekezaji inaonekana hawashtuki kutokana na “kubebwa” na maofisa wasiokuwa waaminifu katika serikali.

Pamoja na hayo, pia kuna haja kwa serikali kuendelea kuitupia macho sekta hiyo, kwa jumla ikiwa ni pamojana kuangalia kiwango cha ukusanyaji wa mapato kama kinakwenda sambamba na hali halisi ya makusanyo.

1 comment: