Monday, January 31, 2011

Wafanyakazi mahoteli walia mishahara yao kucheleweshwa kupindukia

WAFANYAKAZI wengi wa mahoteli hulipwa mishahara yao katikati ya mwezi mwengine wa kazi hali ambayo huwasababishia kuishi katika maisha magumu wao na familia zinazowategemea.

Wakizungumza katika mahojiano na mwandishi wa habari hizi, wafanyakazi wa mahoteli yaliyopo ukanda wa mashariki katika mkoa wa kaskazini Unguja, wamesema mara nyingi hulipwa mishahara baina ya tarehe 10-15 ya mwezi mwengine wa kazi.

Walisema sababu ya kuchelewa haijulikani kwani mahoteli yanakuwa yamesheni wageni lakini wanapojaribu kuulizia huambiwa anaetaka kazi astahamili na asietaka aondoke.

Aidha, hata pale inapolipwa mishahara hiyo huwa pungufu, wakimaanisha kuwa mshahara wa mwezi mmoja haulingani na mwezi mwengine.

“Inawezekana ikatokea mwezi mmoja ukalipwa pesa nyingi, mwezi unaofata ukapunjwa kwa kweli hatuji sababu,” alisema Zainab Kombo, mfanyakazi wa jikoni katika hoteli moja iliyopo Kiwengwa.

Hata hivyo, Juma Kombo,alisema kupunjwa huko mara nyingi hufanywa na wahasibu au washika fedha wa mahoteli, ambao mara nyingi huwa ni wazalendo.

“Meneja wa hoteli huwa ameshatenga kiwango maalum cha mshahara wa wafanyakazi lakini wahasibu na washika fedha ndio wanaozikata, kile cha juu huchukua wao. Sisi katika hoteli yetu tumegundua kuwa kuna vocha mbili za mishahara,” alisema.

Lakini baadhi ya wahasibu wa mahoteli waliozungumza na gazeti hili, wamekanusha wakisema kuwa mishahara wanayolipa ndiyo ile iliyokubaliwa wakati wafanyakazi wa wakisaini mikataba, lakini walikiri kwamba wakati mwengine inaweza kushuka kutoka na mahudhurio ya mfanyakazi kazini.

Changamoto hizo pamoja na zile za kunyanyaswa, zimekuwa zikiwafanya wafanyakazi wa mahoteli wakati mwengine kufanya matukio ya wizi na kuwashambulia waajiri wao.

Hivi karibuni, mfanyakazi mmoja katika hoteli moja ya kitalii, alimshambulia mwajiri wake alietajwa kwa jina la Marina baada ya kumtukana na kumfananisha na mnyama.

Katika tukio hilo mfanyakazi huyo alidaiwa kusahau ufunguo kwenye debe la taka na hata baada ya kuomba radhi, bosi huyo aliendelea kumshambulia kwa maneno ya kashfa na kumzaba makofi pamoja na kumchania mkoba wake jambo lililomtia hasira na kuanza kumshambulia mwajiri wake.

Mfanyakazi huyo amefukuzwa kufanya kazi katika hoteli hiyo.

Akizungumzia suala la unyanyasaji, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya wafanyakazi wa utalii, mahoteli, hifadhi, majumbani na kazi nyengine (ZATHOCODAWU), Maalim Makame Launi, amesema wafanyakazi wa mahoteli wamekuwa wahanga wa manyanyaso, kupunjwa mishahara na kutolipwa kwa wakati, kufukuzwa kazi ovyo na kutopewa mikata hali ambayo inakwamisha juhudi za serikali za kuimarisha sekta ya utalii na kupunguza umaskini.

Alisema wamekuwa wakisimamishwa kazi na mikataba yao kuvunjwa wakati mwengine bila sababu za msingi lakini vyama vyao vinashindwa kuwafikia kwa kuwatetea kwa sababu wengi si wanachama.

Kwa upande wake Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Abdilah Jihad Hassan, alisema serikali sasa inakusudia kuwanyang’anya leseni wawekezaji wanaokiuka sheria za utalii.

Nae Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi amesema serikali haitavumilia wawekezaji wasio waaminifu ambao wmaekuwa wakisababisha umaskini kwa wananchi.

Alisema kwa mfano mmiliki wa hoteli ya kitalii ya Venta Club iliyopo Kiwengwa ameitelekeza hoteli hiyo tokea mwezi Machi mwaka uliopita na kuacha madeni makubwa kwa wafanyakazi na watu waliokuwa wakipeleka bidhaa zao linalofikia shilingi milioni 400 pamoja kodi ya shilingi milioni 600.

Tayari vifaa kadhaa katika hoteli hiyo ikiwemo milango vimeibwa ikiaminika kuwa ni jaribio linalofanywa na wafanyakazi waliokuwa wakitumikia hoteli hiyo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mselem Mtulya amethibitisha kukamatwa kwa vitu kadhaa vilivyoibwa katika hoteli hiyo.

Akizungumzaia masuala ya unyanyasaji, Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharif Hamad amesema serikali haiko tayari kuwavumilia wawekezaji wanaowanyanyasa wafanyakazi katika sekta ya utalii.

Alisema serikali haitawavumuliwa wawekezaji wenye tabia hiyo wakiwa wa nje au wa ndani ambapo kwa kufanya hivyo watakuwa wanavunja sheria.

Alisema serikali itatoa ushirikiano mkubwa kwa wawekezaji kuja kuwekeza Zanzibar lakini haitaridhika kuona wafanyakazi wake wakinyanyaswa.

No comments:

Post a Comment