Friday, January 21, 2011

Ni kosa kwa mwari kupata ujauzito hata kwa hiari yake

Na Juma Khamis
SHERIA ya kuwalinda wari na watoto wa mzazi mmoja, ni moja ya sheria nyingi zilizotungwa na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

Sheria hii ilitungwa kutokana na kukithiri kwa matukio ya udhalilishaji wa wari na watoto wadogo, lengo likiwa ni kukomesha unyanyasi huo hapa nchini.

Kabla ya kuja kwa sheria hiyo, idadi kubwa ya watoto na wari walikuwa wakinyanyasika bila ya kuwepo sheria mahasusi ya kuwatetea.

Hata hivyo, licha kuwepo sheria hii, lazima tukiri kwamba bado vitendo vya kuwadhalilisha wari na watoto vimekuwa vikiendelea, huku wari wengi wakipewa ujauzito na kuishia kuolewa huku wakipoteza fursa nyingi muhimu kwa maisha yao, ikiwemo elimu.

Sheria hii inaelezea kwa kina makosa mbali mbali ya jinai ambayo hayakuelezwa na sheria ya makosa ya Jinai (Penal Act No.6 ya mwaka 2004).

Kabla ya kuzungumzia baadhi ya makosa ya jinai katika sheria hii, kwanza tuone maana ya ‘mwari’ kama mmoja ya mlengwa wa sheria hii.

Kwa mujibu wa kifungu cha pili cha sheria hii, mwari ni mwanamke asiepata kuolewa ambaye yuko baina ya umri wa miaka 18 na miaka 21 na asiyepata kuzaa mtoto.

Baadhi ya makosa yanayotambuliwa na sheria hii ni pamoja mwari atakaepatikana na ujauzito ambao ameupata kwa hiari yake.

Adhabu katika kosa hili iwapo atatiwa hatiani ni kutumikia jamii kwa kipindi cha kuanzia miezi mitatu tokea siku aliyojifungua.

Sheria hii pia imebainisha kuwa mtu yeyote atakaehusika na ujauzito wa mwari huyo atakuwa amefanya kosa na pindi atakapotiwa hatiani adhabu yake ni kutumikia Chuo cha Mafunzo kwa kipindi kisichopungua miaka mitatu na si zaidi ya miaka mitano.

Pamoja na adhabu hiyo atatakiwa atoe matunzo kwa mtoto atakaezaliwa na mwari huyo.

Sheria pia imesema kuwa ni jukumu la mwari yeyote atakaekuwa mjamzito kutaja jina la mtu aliempa ujauzito huo na pindi mwari huyo atakataa kutaja jila mtu huyo atakuwa ametenda kosa la jinai na endapo atatiwa hatiani adhabu yake ni kutumikia jamii kwa kipindi cha miezi mitatu.

Hata hivyo, itakuwa ni kinga kwa mwari huyo kama atathibitisha kuwa ujauzito huo ameupata kutokana na kubakwa na watu wengi au mazingira mengine ambayo hakuweza kumtambua mbakaji.

Iwapo mwari huyo kwa makusudi amemtaja mtu tofauti na aliyemsababishia ujauzito huo, na kama mahakama itaridhika amefanya hivyo kwa makusudi, atakuwa ametenda kosa la jinai na akipatikana na hatia atatumikia jamii kwa kipindi cha miezi sita.

No comments:

Post a Comment